Friday 20 September 2013

Qur’ani inapaswa kutawala maisha ya jamii ya Kiislamu


Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu Ayatullah Ali Khamenei amesema kuwa mwongozo wa Qur'ani na mtindo wa maisha ya Kiislamu vinapaswa kutawala katika jamii ya Kiislamu.
Ayatullah Khamenei aliyasema hayo jana alasiri baada ya majlisi ya qiraa ya Qur'ani iliyoendelea kwa kipindi cha zaidi ya masaa matatu. Alisema kuwa kusoma na kuhifadhi Qur'ani Tukufu ni utangulizi na mwanzo wa kufika kwenye jamii inayotakikana ya Qur'ani. Amesisitiza kuwa, mwongozo wa Qur'ani na mtindo wa maisha ya Kiislamu vinapaswa kutawala jamii ya Kiislamu.
Ayatullahil Udhmaa Ali Khamenei amesema kuwa, kusoma na kuhifadhi Qur'ani Tukufu hutayarisha uwanja mzuri wa kuelewa kitabu hicho cha Mwenyezi Mungu na kujipamba kwa maadili yake. Ameongeza kuwa utamaduni wa jamii ya Kiislamu unapaswa kuoana na akhlaki na maadili ya Qur'ani pamoja na mafundisho ya maasumu.
Ameashiria baadhi ya njama za kutaka kuathiri utamaduni, mtindo wa maisha ya jamii na mahusiano yake ya kijamii kwa kutumia utamaduni wa Kimagharibi na akasema: Kufuatwa utamaduni wa Magharibi na watu wengi duniani hakuwezi kuwa kigezo na hoja ya kufuatwa utamaduni huo katika jamii ya Kiislamu.
Amesema dini, akili timamu na semi za maasumina ndiyo vigezo vilivyoainishwa na Qur'ani ambavyo vinapaswa kuwa mizani na kigezo.
Ayatullahil Udhmaa Khamenei ameelezea kufurahishwa kwake na jinsi vijana wanavyovutiwa zaidi na Qur'ani, kusoma na kuhifadhi kitabu hicho na amesisitiza kuwa: Watu wote wa jamii wanapaswa kujenga uhusiano na Qur'ani Tukufu kwa sababu kusoma na kuielewa Qur'ani ni mwanzo wa kutadabari na kuzama ndani ya maana ya aya za kitabu hicho.

No comments:

Post a Comment