Friday 22 June 2012

Hoja za uamsho hazitozimwa na mabomu ya machozi

FFU na JKU wakimpiga mwandamanaji

KIKUNDI cha uamsho cha Zanzibar pamoja na makundi kadhaa yanayopinga Muungano kinasema Tanganyika inaidhulumu Zanzibar.
Baadhi ya wahubiri wake wanaenda mbele zaidi na kudai kuwa Tanganyika imeigeuza Zanzibar kuwa koloni lake. Baadhi ya wahubiri wengine wanaenda mbele zaidi na kudai kuwa matatizo mbalimbali ya kiuchumi na hali ya wananchi wa Zanzibar yanatokana na kuminywa kunakofanywa na Serikali ya Muungano ambayo ndiyo “Serikali ya Tanganyika” vile vile.
Wanasema kwa ufupi kuwa Muungano ulivyo sasa unaionea Zanzibar na unaibana kama koti linavyombana mtu na sasa wakati umefika kwa koti hilo kuvuliwa.
Wanajenga hoja nyingi sana za jinsi gani Zanzibar inadhulumiwa; kuanzia muundo, mgawanyo wa mapato, suala la mafuta, OIC, mambo ya misaada ya kigeni  na hata nafasi mbalimbali za utumishi wa Muungano. Hoja zao ziko wazi na wala hazina kificho.
Wanazitangaza hoja hizo kwenye makongamano na kwa kweli si hoja mpya. Ni hoja hizi hizi ambazo ziliwahi kumletea matatizo Mzee Aboud Jumbe, na ndizo hizi hizi kwa namna yake ziliwaletea matatizo kina Shaaban Mloo na wengine. Ni hoja hizi hizi ambazo zimekuwa zikitolewa mara kwa mara.
Ni mara moja tu kiongozi wa Bara aliwahi kusimama hadharani na kujibu hoja hizi bila kutumia virungu. Mwalimu Nyerere mara zote aliwashughulikia viongozi wa kisiasa wa hoja hizi. Aliwashughulikia kwa sababu wale walioapa kulinda Muungano hawawezi kukaa kimya wakati Muungano unatishiwa na bado wao wakakinga mikono ya kupokea mishahara, posho na mapochopocho ya Muungano!
Nyerere aliwajibu wale wa Tanganyika waliotaka serikali ya Tanganyika katika lile kundi la G55 lililoongozwa na Njelu Kasaka. Na hata hoja ilipofika hadi bungeni Nyerere alijitokeza na kuwajibu na kudai wazi kuwa serikali yetu (ya Muungano ikiongozwa na Mwinyi na Malecela) “imesurrender” yaani imesalimu amri.

Kinachoshangaza na kuchekesha, hajatokea kiongozi yeyote ambaye amewahi kusimama na kujibu hoja hizi zaidi ya kuzidharau, kuwapiga mkwara na sasa inaonekana hata kujaribu kujibu hakutajaribiwa tena kwani FFU na vyombo vingine vya usalama ndio vitazima hoja kwa nguvu! Wanasiasa wetu wameshindwa!
Ndiyo maana binafsi naamini kuwa kwa vile viongozi wetu wameshindwa kujibu hoja za uamsho hakuna sababu tena ya kutumia vyombo vya usalama kutawanya watu.
Kama mashekhe na viongozi wengine (kama kina Raza na Seif Sharrif) wanaamini kuwa Muungano haufai na wako upande wa Uamsho watoke na wawe wa kwanza kutaka Wazanzibari waamue wenyewe kupiga kura ya maoni. Ni kuchezea watu akili leo kina Seif wanasema ati “Watu wazungumzie Muungano” wakati kinachozungumzwa si “Muungano” tena bali ni “utengano”.


waandishi wa habari wamekuwa wakidanganya umma kuwa wazanzibar wanataka kujitenga. Lakini mimi sikubaliani na hilo. Ninachokijua ni kuwa wazanzibar wanataka muungano ujadiliwe kwa haki bila kuwapanga watanzania kwa madaraja. Yaani watu wa bara wanahaki zaidi ya kujadili muungano kuliko watu wa visiwani. Na kuchagua mambo ya kujidili na mengine nyeti zaidi yasijadiliwe. Hii sio haki mambo yote yajadiliwe kwani Tanzania ni nchi yetu sote.
by Kabavako

No comments:

Post a Comment