Monday 15 February 2016

MATENDO YA MASAHABA KUHUSU SUNNAH

MATENDO YA MASAHABA KUHUSU SUNNAH
Ni jambo maarufu pia kwamba mengi katika matendo ya Masahaba baada ya Mtume (s.a.w.) yalikuwa kinyume cha Sunna yake, kwa hiyo imma Masahaba hawa walikuwa wanaifahamu Sunna ya Mtume (s.a.w.) na waliikhalifu kwa makusudi kutokana na ijtihadi zao dhidi ya Nassi (matamko, matendo na iqrari) za Mtume (s.a.w.), na kwa ajili hiyo Masahaba hawa inawakumba kauli ya Mwenyezi Mungu Mtukufu pale aliposema: "Haiwi kwa Muumini wa kiume wala Muumini wa kike Mwenyezi Mungu na Mtume wake wanapoamua jambo wao wawe na hiyari katika jambo lao, na yeyote mwenye kumuasi Mwenyezi Mungu na Mtume wake basi hakika amepotea upotevu ulio wazi." (Qur'an, 33:36)

Na labda (tuseme) walikuwa hawaijui Sunna ya Mtume (s.a.w.), kwani haistahiki kabisa kwa Mtume (s.a.w.) katika hali kama hii kuwaambia Masahaba wake nimekuachieni Sunna yangu hali yakuwa yeye Mtume anajua kwamba Masahaba wake ambao ni watu wa karibu mno kwake hawaifahamu Sunna yake, basi hali itakuwaje kwa watakaokuja baada yao wakati hata Mtume hawakumfahamu na wala hawakumuona?

Inafahamika pia kwamba Sunna ya Mtume haikuandikwa isipokuwa katika zama za dola ya Bani Abbas, na kwamba kitabu cha mwanzo kilichoandikwa kuhusu hadithi ni "Muwataa" cha Imam Malik, na hiyo ni baada ya fitna kubwa (kupita) baada ya tukio la Karbala na kushambuliwa mji wa Madina, kisha kuuawa kwa Masahaba hapo mjini Madina. Basi ni vipi baada ya matukio hayo mtu atakosa kuwatilia mashaka wasimulizi wa hadithi (za Mtume) ambao walijipendekeza kwa watawala ili waipate dunia? Kwa ajili hiyo hadithi za (Mtume) zimevurugika na kupingana zenyewe kwa zenyewe, nao umma wa Kiislamu umegawanyika kwenye Madhehebu mengi (kiasi kwamba) jambo ambalo limethibiti kwenye madhehebu haya, kwenye madhehebu mengine halikuthibiti, na kitu ambacho kwa hawa wanakiona ni sahihi, wale wanakipinga.
Ni vipi tutaamini kamba Mtume wa Mwenyezi Mungu alisema kuwa "Nimekuachieni kitabu cha Mwenyezi Mungu na Sunna yangu, na hali ya kuwa yeye anafahamu kwamba wanafiki na wapinzani watakuja mzulia?

Hapana shaka Mtume (s.a.w.) alipata kusema,"Wako wengi wenye kunizulia, basi yeyote mwenye kunizulia na ajiandalie makazi yake motoni".
Hivyo basi iwapo wazushi walikuwa wengi katika zama za uhai wake, ni vipi Mtume aulazimishe umma wake kufuata Sunna yake na hali hawaifahamu Sunna iliyo sahihi kutokana na ile isiyo sahihi na dhaifu kutokana na ile yenye nguvu?

Katika hali hii endapo kama Mtume angekuwa ametuachia Qur’an na Sunnah pekee ndio miongozo yetu, basi tungeangukia pua kwa sababu licha ya Qur’an kuwa haina shaka lakini mwenziwe amesheheni uongo na uzushi kiasi kwamba hatuwezi kutofautisha kati ya Sunnah na uongo.
Alhamdulillah baadhi ya waislamu tumeligundua hilo na kuchukua hatua, nayo sio nyingine bali kushikamana na Ahlulbayt wa Mtume ili watuonyeshe Sunnah sahihi kwa sababu Mtume amesema watu hawa wako pamoja na haki na haki iko pamoja nao. 

No comments:

Post a Comment