Tuesday 27 May 2014

UCHUMI WA UARABUNI KABLA YA UISLAMU

Kiuchumi, Wayahudi ndio waliokuwa viongozi wa Arabia. Walikuwa ndio wenye ardhi nzuri yenye kulimika katika Hijazi, na walikuwa wakulima wazuri zaidi nchini humo. Walikuwa pia ndio wawekezaji wa vile viwanda vilivyokuwepo katika Arabia wakati huo, na walikamata ukiritimba wa utengenezaji wa zana za kivita.
Utumwa ulikuwa ni asisi ya kiuchumi ya Waarabu. Watumwa wa kiume na wa kike waliuzwa na kununuliwa kama wanyama, na waliunda tabaka la waliokandamizwa zaidi katika jamii ya kiarabu.
Tabaka lenye nguvu zaidi, la waarabu, liliundwa na mabepari na wakopeshaji fedha. Viwango vya riba walivyotoza kwenye mikopo vilikuwa vikubwa mno, na viliundwa maalum kuwafanya matajiri zaidi na zaidi, na wale wakopaji kuwa masikini zaidi.
Vituo maarufu zaidi vya mjini katika Arabia vilikuwa Makka na Yathrib, vyote katika Hijazi. Wakazi wa Makka zaidi walikuwa ni wafanyabiashara, wachuuzi na wakopeshaji wa fedha.
Misafara yao ilisafiri wakati wa kiangazi kwenda Syria na wakati wa kipupwe kwenda Yemen. Walisafiri pia kwenda Bahrain upande wa Mashariki na Iraq upande wa Kaskazini Mashariki. Misafara ya biashara ilikuwa msingi wa uchumi wa Makka, na kuiendesha kwake kulihitaji ujuzi, uzoefu na uwezo.
R.V.C. Bodley asema:
"Kuwasili na kuondoka kwa misafara kulikuwa ni matukio muhimu katika maisha ya watu wa Makka. Karibu kila mmoja ndani ya Makka alikuwa na namna ya kitega uchumi katika ile mali ya maelfu ya ngamia, mamia ya watu, farasi na punda walioondoka na ngozi za wanyama, zabibu kavu na minara ya fedha na kurudi na mafuta, manukato na bidhaa mbalimbali kutoka Syria, Misri na Fursi (Persia/Iran), na viungo na dhahabu kutoka upande wa Kusini."
(The Messenger, 1946, Uk. 31)
Huko Yathrib, Waarabu waliendesha maisha yao kwa kilimo na Wayahudi waliendesha maisha yao kama wafanyabiashara na wanaviwanda. Lakini Wayahudi hawakuwa wafanyabiashara tu na viwanda; miongoni mwao pia walikuwepo wakulima wengi, na waliileta ardhi nyingi mbovu kwenye kulimika. Kiuchumi, kijamii na kisiasa, Hijazi ilikuwa ndio sehemu mashuhuri zaidi katika Arabia mwanzoni mwa karne ya saba.

Francesco Gabrielli anasema:
"Katika mkesha wa Uislamu, watu wenye kujishughulisha mno na walioendelea wa Arabia waliishi katika mji wa Maquraish. Wakati wa himaya za Arabu ya Kusini za Petra na Palmyra ulikuwa umepita kwa muda kiasi katika historia ya Arabia. Sasa hali ya baadae ilikuwa inaandaliwa hapo katika Hijazi."
(The Arabs - A Compact History-1963)
Waarabu na Wayahudi wote walikula riba. Wengi miongoni mwao walikuwa wala riba wajuzi; waliishi kwa riba waliyotoza kwenye mikopo yao.
E.A.Belyaev anaeleza:
"Riba ilitumika sana Makka, kwani ili kushiriki katika msafara wenye faida, watu wa Makka wengi waliokuwa na kipato cha wastani walikimbilia kwa wala riba; mbali na riba kubwa, angeweza kutegemea kupata faida baada ya kurudi salama kwa msafara. Wafanyabiashara matajiri zaidi walikuwa wachuuzi na wala riba.
Wakopeshaji fedha kwa kawaida walichukua dinari kwa dinari, dirham kwa dirham, kwa maneno mengine, asilimia mia moja ya riba. Katika Qur'an 3:125, Allah (s.w.t.) akiwaambia waumini, alisema: 'Msile riba mara mbili maradufu.' Hii ingeweza kumaanisha kwamba riba ya asilimia mia mbili au hata mia nne ilidaiwa.
Nyavu za riba ya Makka hazikuwakamata wakazi wenzao tu na wa makabila yao bali pia watu wa makabila ya KiBedui ya Hijazi walioshugulika katika biashara ya Makka. Kama katika Athens ya zamani "njia kuu za kukandamiza uhuru wa watu zilikuwa ni pesa."

(Arabs, Islamu and the Arab Caliphate in Early Middle Ages, 1969)

No comments:

Post a Comment