Wednesday 23 April 2014

MASAHABA NA MSIBA WA ALKHAMISI

Ibn Abas anasema kuwa, “Siku ya Alhamis, hiyo siku ya Alhamis ilikuwa na tukio gani? Mtume wa Mwenyezi Mungu yalimzidia maumivu yake akasema, njooni nikuandikieni maandiko ambayo hamtapotea baada yake. Umar bin Khatab akasema Mtume anaweweseka kwa kuzidiwa na maradhi, nanyi mnayo Qur’an, Kinatutosha kitabu cha Mwenyezi Mungu, basi hapo watu waliokuwepo ndani ya nyumba ya Mtume wakakhitilafiana na kuzozana juu ya kuandikiwa wosia. Wapo waliotaka wasogee ili Mtume awaandikie wosia na wapo waliopinga na kusema kama alivyosema Omar bin Khatab kuwa Qur’an inawatosha. Masahaba walipozidisha zogo Mtume akawafukuza”.
Ibn Abas anasema, huu ndio msiba mkubwa kuliko yote katika Uislamu kwani Masahaba walimzuia Mtume wao kuandika wosia.
Soma: Sahihi Muslim, Juz. 5 uk. 75 mwishoni wa kitabul-wasiyyah.
Mpaka hapa nashangazwa na msimamo wa Umar bin Khatab dhidi ya amri ya Mtume Mohammad (S.A.W) juu ya kuulinda umma usipotee na bila shaka maandishi hayo yangesaidia kuondoa khitilafu baina ya waislamu.
Hivi Omar anaposema kuwa ninyi mnayo Qur’an, nayo inatutosha anamaana gani? Je, Omar anafahamu Qur’an zaidi ya Mtume Mohammad (S.A.W.W)? Hili haliwekani bali tabia ya Omar ni kumpinga Mtume kwa kila maagizo ayatoayo kwa waislamu. Nadhani unakumbuka msimamo wa Masahaba katika sulhu ya Hudaibiyyah ambapo Omar aliongoza uasi dhidi ya Mtume wetu kwa mara nyingine.
Lakini kama kweli walifahamu kuwa Mtume anaweweseka, kwa nini alipowafukuza chumbani walitoka? Hii inamaana kuwa waligoma kumruhusu Mtume kuandika wosia kwa sababu walijua Mtume alitaka kuandika nini na hivyo wakaona wamzue kuandika ili wafanye wanavyotaka pindi atakapofariki dunia.
Matendo haya ya Omar bin Khatab yanapingana na Qur’an 49:2 isemayo, “Enyi mlioamini msipaze sauti zenu juu ya sauti ya Mtume na wala msisemezane naye kwa sauti ya nguvu kama mnavyosemezana ninyi kwa ninyi, visije vitendo vyenu vikakosa thawabu na hali ya kuwa hamtambui”.
Katika tukio hili walivuka mipaka ya kupaza sauti na kumsemesha kwa nguvu hadi wakamtuhumu Mtume kwa kuweweseka. Waislamu nakuombeni mjitenge mbali na watu walioongoza fitina ndani ya Uislamu na kumdhulumu Mtume wetu kwa kumzuia kuuongoza Uislamu kwa misingi aliyoagizwa na Mola wake. Pia jitengeni na watu wanaoongoza kwa kutenganisha watu kwa kuwasingizia waislamu wengine kuwa ni makafiri ili wapate sababu ya kuwaua.

No comments:

Post a Comment