Friday 16 August 2013

DUA ILI ALLAH ATUONGOZE TUJUE NA KUFUATA KUNDI SAHIHI



Ewe Mwenyezi Mungu wanadamu tumekhitilafiana na kuwa Wayahudi, Wakristo na Waislamu, ama wayahudi wamekhitilafiana na kuwa makundi 71, Wakristo wamekhitilafiana na kuwa makundi 72, waislamu nao wamekhitilafiana na kuwa makundi 73 na yote yamo katika upotofu isipokuwa kundi moja tu, Kama alivyosema Mtume wako Mohammad (S.A.W.W). Je huu ndio utaratibu uliouweka kama wanavyosema baadhi ya waislamu kuwa Wewe ndiwe uliyeiandikia kila nafsi ikiwa bado tumboni mwa mama yake; iwe Yahudi, Mkristo, Muislamu, mwizi, mshirikina, mlafi, mcha Mungu, muuaji, mchawi n.k. na hatimaye mtu akawa hivyo alivyo?
Kwa hakika nafsi yangu haikubali fikra hizi ya kwamba Qadhaa na Qadar ndiyo iliyoamua hatima ya mtu kimatendo yake, bali karibu nikate shauri kwamba wewe Mwenyezi Mungu ndiwe uliyetuumba, ukatuongoza na ukatufahamisha mabaya na mema, ukatuagiza tufanye mema na kuacha mabaya, na ukawatuma Mitume wako ili watubainishie yanayotutatiza na watujulishe haki kutokana na batili lakini mtu mwenyewe ndiye aliyezugwa na maisha ya dunia na mapambo yake akasahau maelekezo yako.
Kwa ubinafsi na ujeuri wake, kwa ujinga wake na kujitosa kwake katika mambo yasiyo na faida, na kwa inadi yake na uhasama wake, na kwa dhulma yake na kuvuka kwake mipaka, ameiacha haki na kumfuata shetani na akajitenga na wewe Muumba wake. Bila shaka Qur’an tukufu imekwisha lieleza hilo, “Kwa hakika Mwenyezi Mungu hawadhulumu watu kitu chochote lakini watu wanajidhulumu wenyewe (10:44).
Na Mtume wako alitutahadharisha sana pale aliposema, “sio halali kwa muislamu kumnunia ndugu yake muislamu zaidi ya siku tatu,” lakini bado tumegawanyika na kuwa vidola vidogo vidogo vinavyofanyiana uadui vyenyewe kwa vyenyewe na kupigana wao kwa wao.
Umma huu unanini ewe Mwenyezi Mungu, baada ya kuwa ulikuwa umma bora kuliko umati zote na ulipata nguvu duniani na kuwafikishia watu uongofu, elimu, maarifa na maendeleo, ghafla leo hii umekuwa ni umma mdogo na dhaifu mno, ardhi yao imeporwa na wananchi wake wametawanyika na msikiti wao mtakatifu umekaliwa na kupokonywa na wazayuni na wala hawawezi kuukomboa. Hivi na hii nayo umetuandalia tuwe hivi? La hasha kwani fikra inapingana na malengo wako matukufu ya kuuinua Uislamu ili uiongoze dunia. Naomba ewe Mola wangu kama fikra zangu ni sahihi niimarishe katika fikra hizi na niweke pamoja na watu wenye fikra kama zangu. Na kama nimepotoka ninakuomba uniongoze njia iliyonyooka kwani wewe ndiye mbora wa waongozaji.

No comments:

Post a Comment