Tuesday 10 June 2014

MAANA YA MASAHABA KWA UPANDE WA SHIA IMAMIYA

Kwa upande wa Shia, neno sahaba halina maana ya kistilahi kama lilivyo kwa Sunni. Kwa hivyo wao hulitumia neno hili kama linavyotumika kilugha.
Kwa mujibu wa lugha ya_Kiarabu (taz. Lisanul Arab na Mufradat ar-Raghib chini ya neno 'sahaba'), neno sahaba ni wingi wa neno sahib. Na neno sahib maana yake ni 'mwenye kuingiliana na kushikamana na (mwingine).' Wala neno hilo 'hatumiliwi isipokuwa yule ambaye mshikamano wake  (na mwenziwe) ni mwingi.' Na ili kuwa sahib wa mtu yahitajia 'kukaa naye kwa muda mrefu.' Pia kwa kuwa suhba (usahibu) huwa ni baina ya wawili, neno hili — katika sentensi—siku zote huunganishwa na jina moja au jingine; na hivyo ndivyo lilivyotumiwa katika Our'ani Tukufu: k.m. sahibayis sijn (Sura 12:39) na as'habu Musa (Sura 26:61); na katika zama za Bwana Mtume s.a.w.w. pia: k.m. sahibu rasulillahi au as'haburasuli llahi.
Kwa hivyo kwa Shia 'sahaba wa Mtume s.a.w.w.' ni yule anayetimiza yaliyotajwa katika taarifa ya neno hilo hapo juu.
Daraja yao
Baada ya kuona jinsi taarifa ya neno sahaba inavyotofautiana, baina ya Sunni na Shia, tumebakiwa na swali moja; nalo ni: jee, wote ni waadilifu? Wote wamehifadhiwa na kufanya makosa?
Majibu ya Sunni hapo ni: Ndiyo; sahaba wote ni waadilifu, na wote wamehifadhiwa na kufanya makosa. Hivyo ndivyo anavyotwambia Sheikh M. al-Khatib katika kitabu chake.
Lakini Shia wasema: La; sio hivyo. Na wana hoja zao ambazo, japo kwa muhtasari, tumezidondoa katika mjadala huu, na ambazo tafadhali zitazame na uzizingatie. Juu ya hoja hizo, kuna na nyingine mbili:
(i)  imani hiyo inapingana na misingi
inayoelezwa katika Qur'ani Tukufu kuhusu wale waliokuwa karibu zaidi na Mitume wa Mwenyezi Mungu kwa jumla kuliko sahaba zao, na Mtume Muhammad s.a.w.w. hasa kuliko sahaba zake; na
 (ii) inapingana na maumbile ya Binadamu yalivyo.
Inavyopingana na Qur'ani Tukufu
Tunapozingatia kwa makini taarifa ya Kisunni, tunaona kwamba kitu cha pekee kililchofanya sahaba wapawe daraja waliyopawa ya utakatifu, na kuhifadhiwa na kufanya makosa, ni kule kuwa karibu na Mtume s.a.w.w. na kuweza kumwona-japo ni kwa mbali! Hakuna jingine.
Kama ni hivyo basi, hilo halitoshi. Maana tunapoisoma Qir'ani Tukufu tunaona watu waliokuwa karibu zaidi na Mtume Muhammad s.a.w.w. kuliko walivyokuwa sahaba zake kwake, na hata wale wa Mitume wengine, na bado Mwenyezi Mungu hakuwapa daraja ambayo sahaba wamepawa na kina Sheikh M. al-Khatib! Bali tunaona jinsi wanavyo onywa na kukemewa! Kwa mfano:
(i) tunapofungua Sura 11:45-46, tunasoma: 'Nuhu akamlingana Mola wake. Akasema: Mola wangu! Hakika mtoto wangu ni katika watu wangu; na hakika ahadi Yako ni kweli, na Wewe ni Mbora wa wenye kuhukumu.  (Mwenyezi Mungu) akasema: Ewe Nuhu! Hakika huyo si katika watu wako. Yeye ni (mwenye) mwendo usiokuwa mwema. Basi usiniombe usilokuwa na ujuzi nalo. Mimi nakunasihi usiwe miongoni mwa wajinga.'
Jee, kama mkuruba tu na Mtume wa Mwenyezi Mungu ndio unaompa mtu utakatifu, yuko aliye karibu zaidi kuliko mtoto wa kumzaa mwenyewe? Mbona hapo Mwenyezi Mungu anamwambia Mtume Wake, Nuhu a.s., kwamba huyo mtoto wake si miongoni mwa watu wake? Kama mtoto wa Mtume wa Mwenyezi Mungu aweza kuambiwa kuwa hayumo miongoni mwa watu wake, kwa sababu tu amemwasi babake, vipi tunawapa utakatifu sahaba (hata kama maasia yao yamethubutu) kwa sababu tu walimwona Bwana Mtume s.a.w.w.? Jee, aliyetokana na damu ya Mtume wa Mwenyezi Mungu, na aliyemwona tu, yupi yuko karibu naye zaidi?
Pengine wanafunzi wa Mawahhabi watatwambia kuwa mtoto wa Nabii Nuhu a.s. alikuwa kafiri. Kwa hivyo si sawa kumlinganisha na sahaba waliokufa wakiwa Waislamu. Sawa! Jee, Mwana Fatima, binti ya Mtume Muhammad s.a.w.w.? Hakuwa Mwislamu? Hakumwona Bwana Mtume s.a.w.w.? Hakufa katika Uislamu? Kama alikuwa na yote hayo, juu ya kuwa alikuwa kipenzi cha babake, kwa nini babake s.a.w.w. akamwambia (kama tuelezwavyo katika Hadith mashuhuri): 'Niombe unachotaka katika mali yangu. Lakini, kwa Mwenyezi Mungu, mimi sitokufaa kitu'? Au kwa nini Bwana Mtume s.a.w.w. kusema: 'Naapa kwa Mwenyezi Mungu! Lau Fatima binti Muhammad angaliiba, ningalimkata mkono wake'? Jee, hayo yote si kuonyesha kwamba kuwa karibu na Mtume wa Mwenyezi Mungu peke yake hakutoshi, kama hakukuandamana na amali njema? Kama Mwana Fatima a.s. anaambiwa kwamba kitakachomfaa kwa Mola wake ni amali yake, na kwamba akiasi ataadhibiwa, vipi na kwa kipimo gani tunawapa utakatifu huo sahaba kwa sababu tu walimwona Bwana Mtume s.a.w.w.? Na hata kama maovu ya baadhi yao yamethubutu?
(ii) tunapofungua Sura 66:10-11, tunasoma: 'Mwenyezi Mungu amepiga mfano wa wale waliokufuru -mke wa Nuhu na mke wa Luti. Walikuwa chini ya waja Wetu wawili wema miongoni mwa waja Wetu; lakini (wanawake hao) wakawafanyia hiana hao (waume zao), na wao (hao waume) hawakuweza kuwafaa chochote kwa Mwenyezi Mungu. Pakasemwa: Uingieni Moto pamoja na wenye kuuingia. Na Mwenyezi Mungu amepiga mfano (mwingine) wa wale walioamini mke wa Firauni; pale aliposema: Mola wangu! Nijengee Kwako nyumba katika Pepo, na uniokoe na Firauni na vitendo vyake (viovu), na uniokoe na watu madhalimu.'
Haya! Hao hapo wake wawili wa Mitume wa Mwenyezi Mungu: Nabii Nuhu a.s. na Nabii Luti a.s. Kwa sababu hawakuwa na mwendo mzuri, ukuruba wao na Mitume hao haukuwafaa kitu, bali watatiwa Motoni! Sasa ikiwa ni hivyo kwa wake wa Mitume, kwa nini tuambiwe haiwi hivyo kwa rafiki (sahaba) zao?

Kwa nini tuambiwe tusiwatuhumu sahaba kwa ubaya hata kama wamefanya ubaya? Angalia kwenye aya hizo jinsi Mwenyezi Mungu alivyomhukumu kwa wema mke wa mtu mwovu mno (Firauni), akawahukumu kwa uovu wake wa watu wema mno (Mitume)! Yote hayo ni kutuonyesha kwamba kuwa karibu na mtu mwema hakufai kitu kama wewe mwenyewe si mwema, kama ambavyo kuwa karibu na mtu mwovu hakudhuru kitu kama wewe mwenyewe si mwovu. Na hivyo ndivyo inavyotakikana tuwapime sahaba wa Bwana Mtume s.a.w.w. Wale waliothubutu kuwa ni wema, tuwape haki yao. Na wale waliothubutu kuwa ni waovu, tuwape stahili yao. Hivyo ndivyo Kishia, na ndivyo ki-Qur'ani, kama tunavyoona. Maana kama ukuruba peke yake haukuwafaa watoto na wake za Mitume wa Mwenyezi Mungu, walio karibu zaidi nao, vipi utawafaa sahaba zao kwa sababu tu waliwaona?

No comments:

Post a Comment