Wednesday 11 June 2014

NAFASI YA DINI KATIKA JAMII NA TAMADUNI 2

Ama katika amri za kimaumbile mhusika mkuu ni Allah (s.w), kwani amri za kimaumbile na zile sifa na nyenendo maalumu za kimaumbile zenye msukumo wa kimaumbile usiohitajia hiyari, bali inawezekana kukawepo baadhi ya nyenendo za kimaumbile ambazo mwanaadamu anaweza kuzizuia na kuzipeleka katika njia nyingine kwa kiasi fulani, huku Mitume wakionekana kuwa na nguvu za moja kwa moja katika kuzisarifu zile nyenendo zote za kimaumbile kwa idhini ya Mola Mtakatifu.
1. Kwa hiyo, dini ni kitu ambacho uhakika wake tayari uko wazi na ni wenye kutambulika, uhakika ambao umekusanya ndani yake mfumo mzima wa maisha ya mwanaadamu kijumla jumla, na sio kwa ajili ya kikundi au watu maalumu.
 Sio jambo lenye kukubalika kuwa dini ni fikra maalumu za watu, wawe wanasiasa au wana elimu mbali mbali, kwa hiyo ni Mwenyeezi Mungu tu anayeweza kutengeneza dini, na dini tayari imeshatengenezwa kwa mujibu wa maisha na mahitajio ya wanaadamu, ni jambo lilsiloingilika akilini kuwa watu waende kutafuta dini, kwa sababu dini iko tayari, na ni wadhifa wa kila mwanaadamu kufuata dini na sio kutengeneza, mfumo wa haki wa dini ni wa Allah (s.w) na sio watu wengine. Natija tunayoipata kutokana na maelezo hayo ni kuwa :-
*Dini ni mjengeko uliopangwa kwa nidhamu maalumu katika kipindi chote cha historia, kuanzia wakati alipoumbwa mwanaadamu hadi zama hizi tunazokwenda nazo, dini imetumwa kwa watu kwa ajili ya kuwapa uwezo wa kufahamu mambo mbali mbali yanayohusiana na maisha yao, na mambo mengine yote, dini ambazo zimekuja kwa mujibu wa fikra au mifumo ya wanaadamu hizo sio dini za Mwenyeezi Mungu na dini hizo zitakuwa ni nakisi na zenye upungufu, kwa hiyo dini hizo sio sahihi.
Ikiwa patatokea – mbali na Mitume na Ahlulbayt- mtu atakayekuja na madai au ujumbe wa kudai kuwa ujumbe huo amepewa na Mwenyeezi Mungu, au ana uhusiano fulani na Mwenyeezi Mungu basi mtu huyo hana dini, na hana mfumo wowote unaonasibiana na mfumo wa dini aliyoileta Mwenyeezi Mungu (s.w).
Dini ni mfumo na mjengeko uliopangwa kwa nidhamu maalumu, kwa ajili ya watu wote duniani katika kipindi chote cha historia ya binaadamu, Mwenyeezi Mungu ameitengeneza dini na kuwapelekea waja wake kulingana na mahitajio yao ya kila siku, kuanzia zama za Nabii Adam (a.s) hadi zama atakazodhuhuru kiongozi muokozi wa Waislamu, hadharati Mahdi Ajjala llahu Taala Sharifu.
Dini ni mfumo maalumu wa elimu, hukumu, na taaluma mbali mbali za kitabu kitukufu cha Wahyi wa Mwenyeezi Mungu (Qur-an) , ndani ya kitabu hicho kuna mabainisho mbali mbali ya mambo yaliyopita, mambo yaliyopo, yajayo na mambo yatakayokuja, ndani ya kitabu hicho mna kila kitu anachokihitajia mwanaadamu na viumbe wote kwa ujumla cha dhahiri na cha batini. Natuangalie Aya hii tukufu ya Mwenyeezi Mungu iliyonukuliwa na mmoja wa Maimamu maasumu (a.s) Yeye kuhusiana na dini anasema hivi:-
Funguo za kila elimu ziko kwake Yeye Mola Mtakatifu, na anayathibitisha hayo kupitia kauli yake Allah (s.w)
Yeye (s.w) anasema:-
" وَعِندَهُ مَفَاتِحُ الْغَيْبِ لاَ يَعْلَمُهَا إِلاَّ هُوَ وَيَعْلَمُ مَا فِى الْبَرِّ وَالْبَحْرِ وَمَا تَسْقُطُ مِن وَرَقَةٍ إِلاَّ يَعْلَمُهَا وَلاَ حَبَّةٍ فِى ظُلُمَاتِ الاَرْضِ وَلاَ رَطْبٍ وَلاَ يَابِسٍ إِلاَّ فِى كِتَابٍ مُّبِينٍ[3]".
Na ziko kwake funguo za ghaibu; hakuna azijuaye ila Yeye tu. Na Yeye anajua kilioko nchi kavu na baharini. Na halidondoki jani ila analijua. Wala punje katika giza la ardhi, wala kinyevu, wala kikavu ila kimo katika Kitabu kinachobainisha.
Maana na ufafanuzi wa Aya hiyo ni kama ifuatavyo:-
Vitu vyote duniani vilivyo na uhai na visivyo na uhai vimedhibitiwa ndani ya Qur-an na viko katika milki yake Yeye Allah (s.w), yaani rikodi ya kila kitu iko kwa Allah (s.w).
Kuwepo kwa Qur-ani kwa ajili ya dini ya Kiislamu, na pasitokee na mtu yeyote atakayeweza kukiharibu au kukiharifu kitabu hicho, yote hayo yanathibitisha uwezo wake Allah (s.w) katika kuihifadhi dini na kitabu chake kitukufu. Ikiwa patatokea mtu awezae kuipunguza au kuizidisha herufi angalau moja ya Qur-an  (na hakuna anayeweza wala atakayeweza kufanya hivyo) basi kitabu hicho hakitakuwa kitabu cha Wahyi wa Mwenyeezi Mungu, wala hakitakuwa kitabu cha dini.
Ufafanuzi wa paragrafu hiyo ni kwamba:-
Mwenyeezi Mungu amekiteremsha kitabu cha Qur’an kikiwa ni nyenzo ya kumuongoza mwanaadamu katika saada kwa kufanya yale aliyoamrishwa na Mola wake kupitia kitabu hicho, na kwa muongozo wa Mitume ya Mwenyeezi Mungu na Ahlulbayt (a.s), kwa hiyo kama tukisema kuwa kitabu hicho kina upungufu au kimezidishwa baadhi ya mambo ambayo Mwenyeezi Mungu hakuyatia mambo hayo katika kitabu hicho, itamfanya mwanaadamu awe na udhuru wa kumshitakia Mola wake kuwa yale aliyomtaka ayafanye yalizidishwa au kupunguzwa katika kitabu hicho ambacho kilikuwa ndio muongozo wake.
Tunaweza kuufafanua ufumbuzi wa dini katika njia mbili zifuatazo:-
1. kwa kuifanyia uhakiki nafsi ya mwanaadamu mwenyewe.
2. Katika ulimwengu wa MIYTHAAQ (میثاق).
Ulimwengu wa Miythaaq unarejea katika kile kipindi ambacho Mwenyeezi Mungu alimuumba mwanaadamu. Pale Allah (s.w) alipowauliza waja wake,
 وَإِذْ اَخَذَ رَبُّكَ مِن بَنِى آدَمَ مِن ظُهُورِهِمْ ذُرِّيَّتَهُمْ وَاَشْهَدَهُمْ عَلـٰي اَنفُسِهِمْ اَلَسْتَ بِرَبِّكُمْ قَالُواْ بَلَي شَهِدْنَا اَن تَقُولُواْ يَوْمَ الْقِيَامَةِ إِنَّا كُنَّا عَنْ هَذَا غَافِلِينَ[4]
Na pale Mola wako Mlezi alipo waleta katika wanaadamu kutoka migongoni mwao kizazi chao, na akawashuhudisha juu ya nafsi zao, akawaambia: Je, Mimi si Mola Mlezi wenu? Wakasema: Kwani! Tumeshuhudia. Msije mkasema Siku ya Kiyama sisi tulikuwa tumeghafilika na hayo.
Maelezo kuhusiana na Aya:-

Mradi wa Aya hii ni kuwa; Mwenyeezi Mungu amemtia kila Binaadamu ujuzi wa kujitambua kuwa yeye ameumbwa, na yuko aliyemuumba, na huyo ndiye Mwenyeezi Mungu. Basi hana hoja ya kusema kuwa alipotezwa na wazee wake wala nani. Sio hoja hiyo kwani kila mmoja amepewa akili na utambuzi, kwa nini anajifuatia tu.

No comments:

Post a Comment