Friday 12 September 2014

MAOMBI YANGU KWA MAWAHHABI

Nakuiteni kwenye Kitabu cha Mwenyezi Mungu, na sunna ya Mtume wake, semeni kweli wazi wazi kwa sauti kubwa japokuwa ni chungu itakushuhudieni mbele ya Mwenyezi Mungu.
Naapa kwa Mola wako hivi kwenu ninyi Mashia siyo Waislamu? Hivi kweli mnaitakidi kwamba wao ni makafiri? Je wafuasi wa Watu wa nyumba ya Mtume ambao wanampwekesha Mwenyezi Mungu na kumtukuza zaidi kuliko vikundi vyote kwa usemi wao wa kuwa hafanani na chochote kwa kumtakasa kutokana na kufanana, na kutokana na kuwa hana umbo na mwili. Si hivyo tu bali wanamuamini Mtume wake Muhammad (s.a.w.w.) na wanamuheshimu mno kuliko vikundi vyote wasemapo kuwa, "Yeye Mtume ni Maasum moja kwa moja hata kabla ya kupewa utume". Je, hawa ndiyo munaowahukumu kuwa ni makafiri?
Je, wale wanaomtawalisha Mwenyezi Mungu na Mtume wake na wale walioamini na wanawapenda kizazi cha Mtume na kuwatawalisha kama alivyowatambulisha Ibn Mandhur ndani ya "Lisanul-A'rab" katika mada ya Shia, basi je ninyi mwasema kwamba wao siyo Waislamu?
Je, Mashia hawa ambao wanatekeleza wajibu wa Sala kwa namna iliyo bora, na wanatoa Zaka na kuzidisha juu yake Khumsi ya mali zao kwa ajili ya kumtii Mwenyezi Mungu na Mtume wake na wanafunga (saumu ya) mwezi wa Ramadhani na nyingine na wanahiji nyumba Tukufu ya Mwenyezi Mungu na kuyatukuza mambo matukufu ya Mwenyezi Mungu, kadhalika wanawaheshimu Mawalii wa Mwenyezi Mungu na kujiepusha na maadui wa Uislamu, hivyo kwenu ninyi watu hawa ni washirikina?
Je, hivi watu wasemao kuwa Uimamu hasa ni (haki) wa Maimamu kumi na wawili kutoka katika watu wa nyumba ya Mtume ambao Mwenyezi Mungu amewaondolea uchafu na amewatakasa sana sana, na Mtume wa Mwenyezi Mungu aliwataja kama alivyotoa Bukhari na Muslim na wengineo katika Sahihi za Ahlu-Sunnah, hivi watu hawa kwenu ninyi ni watu waliotoka nje ya Uislamu?
Je hivi kuna siku ambayo Waislamu wamekuwa hawautambui Uimamu na wala hawakubali sawa sawa liwe hilo katika uhai wa Mtume au baada ya kufa kwake mpaka kufikie kuihusisha nadharia ya Uimamu kwa Waajemi na Majusi?
Na je hivi mnasema kwa kujiamini kuwa, "Ni Kafiri asiyekubali Uimamu wa Yazidi ibn Muawiyyah ambaye uovu wake unaeleweka kwa Waislamu wote? Na itoshe uovu na udhalimu wa Yazidi kwa maelezo walioafikiana Waislamu wote kutokana na yeye kuruhusu kufanyika maasi kwenye mji Mtakatifu wa Madina kwa kutumia jeshi lake na askari wake kufanya wayatakayo mjini humo ili wachukuwe viapo vya utii (kutoka kwa watu) kwa nguvu kama kwamba (watu hao) ni watumwa wake. Si hivyo tu, bali wa Yazid waliwaua maelfu ya Masahaba watukufu na Tabiina, wakavunja heshima za wanawake na wasichana wa Kiislamu waliojihifadhi kiasi walizaliwa kutokana na uchafu huo idadi ya watoto ambao hakuna awezaye kuidhibiti isipokuwa Mwenyezi Mungu.

MASHIA NI AKINA NANI,AU NINI MAANA YA SHIA?

Assalaam alaikum:
MASHIA NI AKINA NANI,AU NINI MAANA YA SHIA?:
Shia ni jina amabalo huitwa wale watu wa dhehebu la waislaam ambao hujulikana kihistoria kama "شيعة علي" = SHIAT ALI = "MASHIA WA ALI" yaani (wafuasi wa Ali) au "أتباع علي" = (Wafuasi wa Ali).
Na mara nyingi Istilahi hii inapotajwa huashiria MASHIA AMBAO NI WAFUASI WA MAIMAM KUMI NA WAWILI, na katika Mashia hili ndilo kundi kubwa zaidi ukilinganisha na mashia wengine ambao si wafuasi wa Maimam Kumi na wawili kama mashia wale wanaoitwa Zaidiyya, na Ismailiyya, hawa pia ni Mashia lakini si mashia wenye kufuata Maimam Kumi na wawili bali ni mashia ambao wanaishia kwa Zaidi na Ismaili na ndio maana wakanasibishwa kwa majina hayo wakaitwa Zaidiyya na Ismailiyya.
Hivyo tunaposema Mashia hatumaanishi au kukusudia Mashia Zaidiyya wala Mashia Ismailiyya, bali tunamaanisha wale Wafuasi (Mashia) ambao hufuata Maimam Maasumin Kumi na wawili kutoka katika Kizazi Kitukufu cha Mtume (s.a.w.w) na ambao ndio walioteuliwa na Mtume (s.a.w.w) kuwa Makhalifa na Mawasii baada yake kwa dalili zilizowazi ndani ya vitabu vya kishia na kisunni.
Hivyo: Mashia hawa au wafuasi hawa kwa kuwa wanafuata Maimam 12 wa Ahlul-bait (a.s) ndio maana wakaitwa SHIA ITHNA ASHARI, kwa maana MASHIA au WAFUASI WENYE KUWAFUATA MAIMAM KUMI NA WAWILI.
Na Maimam hao kumi na wawili (12) watwaharifu (a.s) majina yao yametajwa katika Hadithi za Mtume (s.a.w.w) na riwaya mbalimbali zilizopokelewa kwa pande zote mbili au kwa Madhehebu zote mbili yaani: Shia Ithna Ashari na Ahlu Sunna.
Kundi hili la Mashia wenye kuwafuata Maimamu kumi na wawili katika Mashia ndio lenye wafuasi wengi zaidi ukilinganisha na makundi mengine.Hivyo kutokana wingi wa wafuasi wake ndio maana mara nyingi likitajwa neno SHIA basi bongo za watu hujua kuwa wanaokusudiwa ni Mashia Ithna Ashari yaani: WAFUASI WA MAIMAM KUMI NA WAWILI (A.S). Ndio ni neno, la jumla lakini kutokana na wingi wa wafuasi wa Maimam Kumi na wawili neno hilo likitajwa moja kwa moja linawahusu hao wenye kuwafuata Maimam kumi na wawili.
Lakini waliowachache tunaweza kusema hawajui ufafanuzi huu, bali wao wanachokijua ni kundi la Shia, hawajui kuwa Shia ni kama Bahari, maana ukisema bahari lazima uainishe unakusudia bahari ipi, maana kuna bahari ya Hindi, kuna bahari ya Atlantiki, kuna bahari ya Pasific... hivyo ni bora -ikiwa hatutasema ni lazima- ueleweke unakusudia bahari ipi!. Ndio unasema Bahari, lakini bahari ipi umelenga kuikusudia katika katika mazungumzo yako. Na hivyo hivyo kuhusu Shia, ukisema shia unaeleweka umesema Shia, lakini hueleweki umekusudia shia wepi hivyo ni bora useme Shia zaidiyya au Shia Ismailiyya au Shia Ithna Ashari, kama unavyosema Bahari ya hindi, Bahari ya Pasific, na Bahari ya Atlantiki!.

Swali langu kwa Mawahhabi na Matakfir wengine.

Swali langu kwa Mawahhabi na Matakfir wengine.
Na je hivi mnasema kwa kujiamini kuwa, "Ni Kafiri asiyekubali Uimamu wa Yazidi ibn Muawiyyah ambaye uovu wake unaeleweka kwa Waislamu wote? Na itoshe uovu na udhalimu wa Yazidi kwa maelezo walioafikiana Waislamu wote kutokana na yeye kuruhusu kufanyika maasi kwenye mji Mtakatifu wa Madina kwa kutumia jeshi lake na askari wake kufanya wayatakayo mjini humo ili wachukuwe viapo vya utii (kutoka kwa watu) kwa nguvu kana kwamba (watu hao) ni watumwa wake. Si hivyo tu, bali askari wa Yazid waliwaua maelfu ya Masahaba watukufu na Tabiina, wakavunja heshima za wanawake na wasichana wa Kiislamu waliojihifadhi kiasi walizaliwa kutokana na uchafu huo idadi ya watoto ambao hakuna awezaye kuidhibiti isipokuwa Mwenyezi Mungu.
Na yamtosha Yazidi aibu mbaya mno na udhalimu wa kudumu kule kumuuwa Bwana wa vijana wa peponi na kuwateka Mabinti wa Mtume na kuyachokora meno ya Husein (a.s.) kwa kijiti kisha kuimba kwake beti za ushairi ambazo ni maarufu akasema, "Laiti wazee wangu (waliouawa) katika Badri wangeshuhudia..." Mpaka akafikia kusema: "Banu Hashim walichezea Ufalme, hakuna habari yeyote iliyokuja wala Ufunuo ulioshuka."
Ni wazi kabisa kwamba hakuamini utume wa Muhammad (s.a.w.w.) wala Qur'an Tukufu, basi je, ni kweli mnaafiki kumkufurisha anayejitenga na Yazid? Na baba yake Muawiyyah ambaye alikuwa akimlaani Ali (a.s) na huamuru alaaniwe, bali na (alikuwa) akimuuwa kila anayekataa kufanya hivyo miongoni mwa Masahaba wema kama alivyomfanyia Hujr ibn Adiyy Al-Kindi na jamaa zake, na (tendo la kumlaani Ali a.s.) aliliusia likawa ni sunna iliyofuatwa kwa miaka sabini hali ya kuwa (Muawiyyah) anaijua kauli ya Mtume (s.a.w.w.) aliposema "Yeyote atakayemtukana Ali, basi kanitukana mimi, na atakayenitukana mimi amemtukana Mwenyezi Mungu". Kama ambavyo zilivyoandika Sahih za Ahli-Sunnah kwa ziyada ya matendo aliyoyatenda miongoni mwa mambo yanayopingana na Uislamu kwa kuwauwa watu wema wasio na kosa ili achukue kwao kiapo cha utii kwa ajili ya mwanawe Yazid. Vilevile kumuua kwake, Hassani ibn Ali (a.s.) kwa kumtumia Ju'da binti Ash-ath, na maovu mengine mengi yanatajwa na historia kwa Masunni kama ambavyo pia yanashuhudiwa na wafuasi wa Imam Ali (a.s.).
Mim, sikudhani kwamba ninyi mnaafikiana na hayo, vinginevyo basi na tuyaache kama yalivyo, na ikifika hapo basi hapatabakia baada ya hayo kipimo wala akili, wala sheria na wala hekima pia dalili. Na Mwenyezi Mungu anasema: "Enyi mlioamini mcheni Mwenyezi Mungu na kuweni pamoja na wakweli." (Qur'an, 9:119)

ARABIA KABLA YA UISLAMU

Hali ya Kisiasa katika Arabia.
Sura inayoonekana sana ya maisha ya kisiasa ya Arabia kabla ya Uislamu ilikuwa ni kutokuwepo kabisa kwa mfumo wa kisiasa katika muundo wowote ule. Ukiiondoa Yemen iliyoko Kusini Magharibi, hakuna sehemu ya peninsula ya Arabia iliyokuwa na serikali kwa wakati wowote ule, na Waarabu kamwe hawakutambua mamlaka yoyote ile mbali na mamlaka ya machifu wao wa makabila yao. Haya mamlaka ya machifu wa kikabila hata hivyo, yaliegama, kwa namna nyingi, juu ya tabia na nafasi zao, na yalikuwa ya uungwana kuliko kisiasa.
Mwanafunzi wa kisasa wa historia anaona mshangao kwamba Waarabu wameishi, kizazi baada ya kizazi, karne baada ya karne, bila ya serikali ya aina yoyote ile. Kwa vile hapakuwa na serikali, hapakuwa na sheria na utulivu. Kanuni pekee ya nchi ilikuwa ni hali ya uhalifu. Kama inavyotokea, inapofanyika jinai, upande uliodhuriwa ulichukua hatua mikononi mwao, na ukajaribu kupitisha 'hukumu' kwa yule mwovu. Mtindo huu ulisababisha mara nyingi matendo ya ukatili wa kuogofya.
Kama Waarabu walifanya kiasi kidogo cha kujizuia, haikuwa ni kwa sababu ya wepesi wa hisia alizokuwa nazo juu ya maswali ya kweli na batili lakini ni kwa sababu ya kuhofia kuchochea visasi na mauaji ya kurithi kisasi. Mauaji ya kisasi cha kurithi yalimaliza vizazi vizima vya Waarabu. Kwa vile hakukuwepo na vitu kama polisi, mahakama au majaji, ulinzi pekee mtu alioweza kuupata kutokana na maadui zake, ulikuwa katika kabila lake mwenyewe.
Kabila lilikuwa na jukumu la kulinda watu wake hata kama walitenda maovu. Ukabila au 'asabiyya' (moyo wa kiukoo) ulichukua nafasi ya kwanza kabla ya maadili. Kabila lililoshindwa kulinda watu wake kutokana na maadui zao lilijihatarisha kwenye kebehi, kashfa na dharau. Maadili, kwa kweli hayakuingia kwenye picha mahali popote pale. Kwa vile Arabia haikuwa na serikali; na kwa vile waarabu walikuwa na utawala huria kwa silika yao, walifungana katika mapigano yasiyokwisha. Vita ilikuwa ni desturi ya kudumu ya jamii ya kiarabu. Jangwa liliweza kuchukua idadi ndogo tu ya watu, na hali ya vita vya kikabila ilidumisha uthibiti mkali juu ya ongezeko la watu. Lakini Waarabu wenyewe hawakuiona vita katika mwanga huu. Kwao wao, vita vilikuwa burudani au kiasi mchezo wa hatari, au aina ya tamthiliya ya kikabila, iliyofanywa na wenye weledi (ubingwa), kwa mujibu wa mfumo wa kanuni za zamani na ushujaa, ambapo "watazamaji" walishangilia.
Amani ya kudumu haikuwa na mvuto kwao na vita vilitoa fursa ya kukwepa kazi ngumu na kutokubadilika kwa mwenendo wa maisha katika jangwa. Wao kwa hiyo walichochea msisimko wa mapambano ya silaha. Vita viliwapa fursa ya kuonyesha vipaji vyao katika kutupa mishale, ufundi wa kurusha panga na upandaji wa farasi, na pia, katika vita, wangeweza kujipatia sifa kwa ushujaa wao na wakati huohuo kuleta fahari na heshima kwa makabila yao. Kwa mara nyingi, Waarabu walipigana ili kupigana tu, ama iwepo au isiwepo sababu ya kuchochea vita.
Kwa bahati mbaya mpaka leo kuna baadhi ya watu wanaojifanya waislamu wamekuwa na tabia za kupenda vita na kuuwa watu kama ilivyokuwa kabla ya Uislamu. Uislam haujafanikiwa kuwakomboa watu hawa wenye uchu wa kumwaga damu ya waislamu. Kiongozi wa wamwaga damu hawa ni Muhammad ibn Abdul-wahhab aliyeirithi tabia hii mbaya toka kwa Ibn Taimiyyah na Maswahhaba waovu kama Khalid ibn Walid

KWA NINI WAISLAMU WANARUDI KWENYE ENZI YA UJINGA YAANI KABLA YA UISLAM.

KWA NINI WAISLAMU WANARUDI KWENYE ENZI YA UJINGA YAANI KABLA YA UISLAM.
Anasema G.E. Grunebaum:
"Katika karne ya kabla ya kuja Uislamu makabila yalitawanya nguvu zao zote katika vita vya kuviziana, wote dhidi ya wote."
(Classical Islam - A History 600-1258-1970)
Yale makabila ya wahamaji yalizunguka kwenye peninsula yote na kupora misafara na makazi madogomadogo. Misafara mingi na vijiji vilinunua kinga ya mashambulizi Haya kwa kulipa kiwango maalum cha fedha kwa watekanyara wa wahamaji.
Ni muhimu kuzingatia ule ukweli katika usiku wa kuzaliwa Uislamu hakukuwa na serikali katika ngazi yoyote katika Arabia, na ukweli huu unawezakuwa umeathiri kuinukia kwa Uislamu wenyewe. Ukosekanaji mzima wa serikali, hata katika hali ya kuanzishwa tu, ni kitu kisichokuwa cha kawaida kabisa kwamba kimeonwa na kutolewa maoni na mus-tashirik wengi, miongoni mwao ni:
D.S. Margoliouth:
"Arabia ingebakia ya kipagani angekuwapo mtu katika Makka ambaye angeweza kutoa pigo; ambaye angeweza kutenda. Lakini wengi wao, kama walivyokuwa wabaya wa Mohammed, hapakuwa na mmoja wao aliyekuwa na ujasiri wa namna hii; na (kama ilivyoonekana) hapakuwepo na mahakimu kwa ujumla ambao kwao angeweza kushitakiwa."
(Mohammed and the Rise of Islam, 1971).
Naye Maxime Rodinson asema:
"Mauaji ya halaiki yalibeba adhabu kubwa kwa mujibu wa sheria zisizoandikwa za jangwani. Katika utendaji waarabu huru walikuwa hawakufungwa na kanuni ya sheria zake kwa msaada wa jeshi la polisi. Ulinzi pekee wa maisha ya mtu ni ile hakika iliyowekwa na mila na desturi, ambayo ingenunuliwa kwa gharama kubwa. damu kwa damu na uhai kwa uhai. "
(Mohammed, 1971) Asema Herbert J. Muller:
"Katika Arabia ya Mohammed hakukuwa na dola kulikuwa tu na makabila huru yaliyotangaa na miji. Huyu Mtume (s.a.w.) aliunda dola yake mwenyewe, na aliipa sheria tukufu iliyoandikwa na Allah (s.w.t.)"
(The Loom of History, 1958)
Watu wa Arabia walitokana na makundi mawili, wenye maskani na wahamiaji. Hijazi na Arabia ya Kusini ilitapakaa miji mingi midogo na mikubwa michache. Nchi yote iliyobakia illikuwa na watu waliotapakaa wakitokana na Mabedui. Walikuwa nyuma katika dhana ya uraia na siasa lakini pia walikuwa ni chanzo cha wasiwasi na hofu kwa wale wenye maskani. Waliishi kama maharamia wa jangwani, na walikuwa na sifa mbaya kwa ubinafsi wao usiozuilika na vurugu zao za upambanuzi wa kikabila.
Yale makabila maarufu zaidi yalitumia kiwango maalum cha mamlaka katika maeneo yao husika. Katika Makka kabila lenye nguvu lilikuwa la Quraishi, katika Yathrib, makabila yenye nguvu yalikuwa ni yale makabila ya Kiarabu ya Aus na Khazraji, na makabila ya kiyahudi ya Nadhir, Qaynuqa'a na Quraydha. Maquraishi wa Makka walijiona wenyewe ni bora kuliko Mabedui lakini hawa Mabedui walikuwa na dharau tu juu ya hawa watu wa mjini ambao kwao wao walikuwa ni "Taifa la wauza maduka tu".
Waarabu wote walikuwa na sifa mbaya kwa namna fulani ya tabia kama vile majivuno, kiburi na majisifu, ulipizaji kisasi na kupenda kwingi uporaji. Kiburi chao kilihusika kwa namna fulani na kushindwa kwao kuanzisha dola yao wenyewe. Walikosa nidhamu ya kisiasa, na mpaka kuja kwa Uislamu, hawakutambua mamlaka yoyote kama ni yenye umuhimu mkubwa katika Arabia.
Walitambua mamlaka ya mtu aliyewaongoza kwenye uvamizi lakini angeweza kulazimisha utii wao ikiwa tu walikuwa na uhakika wa kupata mgao mzuri wa ngawira, na mamlaka yake yaliisha mara tu shughuli hiyo ilipokwisha.
CHA KUSHANGAZA KARNE 14 BAADA YA KUWA WAISLAMU, BAADHI YA WAISLAMU WANADESTURI ZILEZILE ZA UJIMA. HAWATAKI KUITII SERIKALI YOYOTE, VISASI NI IBADA KWAO, HAWANA UTII SI KWA VIONGOZI WA SERIKALI BALI HATA MASHEIKH WAO WENYEWE. SI AJABU KUSIKIA MWANAFUNZI AKIMKUFURISHA MWALIMU WAKE. HUU NI MSIBA MKUBWA KATIKA UMMA HUU WA KIISLAMU

Maana ya Ahlu-sunna:

Maana ya Ahlu-sunna:
Kuna maana tatu zinazotafsiri kinachokusudiwa kunako neno Ahlu-sunna,na maana hizo zinapatikana katika vitabu vya wanazuoni wa Kisunni. Na zimekuwa maana tatu kutokana na tofauti iliyopo baina yao kuhusiana na uhakika wa Istilahi hii Ahlu-sunna, lini hasa imeenza na ni nani mwanzilishi wa Istilahi hii.Tunazitaja maana hizo za neno Ahku-sunna kama ifuatavyo:
1-Madh-hebu ya Ahlu-sunna maana yake: Ni kundi la watu wa Hasan Al-basri, walioshikamana na "dhahiri ya Nassu" hata kama dhahiri hiyo inakwenda kinyume au inapingana na akili.
Kwa muhtasari: Maana hii inasema hivi:Ahlu-sunna ni kundi lile la waislaam waliokuwa wakiongozwa na Hasan Al-Basri, ambao hukabiliana na Dhahiri ya Nasu (kama vile kushikamana na dhahiri ya hadithi au Riwaya) pasina kufanya tafsiri wala Taawili, sawa sawa (dhahiri ya Nasu hiyo) iwe inaafikiana na akili au inapingana na kwenda kinyume na akili.
Rejea: Al-firqatun-najia: Juzuu ya 1, Ukurasa wa 405.
2-Madh-hebu ya Ahlu-sunna: Maana yake ni yale madh-hebu aliyoyaasisi Abu Hasan Al-Ash-ari.
3-Madh-hebu ya Ahlu-sunna: Maana yake ni wale waislaam wanaoamini uhalali na haki ya Ukhalifa wa Abubakari na Umar, na Uthman, na kwamba hao watatu ukhalifa wao ni halali na ni haki kutangulia ukhalifa wa Imam Ali bin Abi Talib (a.s). Zaidi ya hilo pia huitikadia kuwa: KHERI NA SHARI VYOTE HUTOKA KWA MWENYEEZI MUNGU (S.W).
Hao ndio huitwa Ahlu-sunna.Kwa maana ikiwa wewe si mwenye kuamini au kuitikadia kuwa Khalifa wa kwanza ni Abubakar, na wa pili ni Omar na wa tatu ni Othman na wa nne ni Ali, bali unaamini na kuitikadia kuwa Khalifa wa kwanza ni Imam Ali Bin Abi Talib (a.s) kwa mujibu wa Nasuu (Hadithi) za Mtume (s.a.w.w), basi wewe hutoitwa kuwa ni katika Ahlu-sunna, na pia ukiwa unaamini kuwa Kheri hutoka kwa Mwenyeezi Mungu (s.w) na Shari haitoki kwa Mwenyeezi Mungu (s.w) bali hiyo ni natija au matokeo ya matendo ya watu, basi pia hilo litakufanya usiitwe au usiwe miongoni wa Madh-hebu hii ya Ahlu-sunna maana utakuwa umeenda kinyume na maana kamili ya neno Ahlu-sunna kama ilivyotajwa katika sehemu hii (namba 3). Maana hii namba tatu ndio maana anayoita mwanazuoni maarufu wa kissuni katika kitabu chake, anayeitwa: Abu Zuhra, na kitabu chake kinaitwa: Tarikh Al-madhahibul-Islamiyya. Na hii ndio maana yenye uzito zaidi kuliko maana zile mbili zilizotangulia.
Rejea: Tarikh Al-madhahibul-Islamiyya: Juzuu ya 2;ukurasa wa 58.

ELIMU MIONGONI MWA WAARABU KABLA YA UISLAMU

Miongoni mwa Waarabu walikuweko watu wachache sana walioweza kusoma na kuandika. Wengi wao hawakuwa na shauku sana ya kujifunza fani hizi. Baadhi ya wanahistoria wana maoni kwamba elimu ya watu ya wakati ule takriban ilikuwa ya simulizi tu. Wayahudi na Wakristo walikuwa ndio watunzaji wa elimu kama hiyo ambayo Arabia ilikuwa nayo.
Elimu ya taaluma kubwa kamilifu ya wapagani wa Kiarabu ilikuwa ni ushairi wao. Walidai kwamba Mungu alijaalia Ubora usiokifani, wa kichwa, juu ya Wagiriki (ushahidi wake ni sayansi na falsafa yao); wa mikono, juu ya Wachina (ushahidi wake ni ufundistadi wao); na wa ulimi kwa Waarabu (ushahidi wake ni ufasaha wao). Fahari yao kubwa, nyakati zote kabla na baada ya Uislamu, ilikuwa ni ule ufasaha wao katika ushairi. Umuhimu wa mashairi unatathminiwa kama ifuatavyo:
(Arabs, Islam and the Arab Caliphate in the Early Middle Ages, 1969)
Mashairi ya Kiarabu yalikuwa na utajiri katika ufasaha na matumizi ya tamathali za usemi katika mazungumzo au maandishi, lakini yalikuwa na ukomo wa masafa, na yalikuwa na upungufu wa maana. Maneno yaliyomo yaweza kuwa ya kuvutia lakini yalikuwa chapwa! Kazi bora za mashairi yao takribani hufuatia kabisa utaratibu uleule wa fikira na mawazo. Hata hivyo yalikuwa ni kioo cha uaminifu katika maisha ya zamani ya uarabuni. Vile vile katika kuchimbua sanaa ya ushairi, washairi wa kiarabu kwa hadhari walikuwa wakiendeleza moja ya sanaa kubwa za binadamu - lugha ya Kiarabu.
Utungaji mkubwa wa mapagani wa Kiarabu ni ule ulioitwa "Golden Odes", mkusanyiko wa mashairi saba, yakidhaniwa ya ubora usiopitwa, yenye nguvu na ufasaha. Yalitundikwa ndani ya Al-Kaaba kama changamoto kwa yeyote mwenye kutamani kuyapita au kulin-gana nayo. Sir William Muir anaandika kuhusu mashairi Haya kama ifuatavyo:
"Mashairi saba yaliyotundikwa yalikuwa hai kuanzia hata kipindi kilichomtangulia Muhammad, kielelezo cha kushangaza cha ufasaha usio hila. Uzuri wa lugha na utajiri wa kuenea haraka wa matumizi ya tamathali za usemi katika mazungumzo na maandishi unakubaliwa na wasomaji wa ulaya, lakini somo la mshairi liliwekewa ukomo, na yale yasiyo ya kawaida yalikengeukwa.
Haiba ya kimada wake, baka la kuonewa wivu lililowekwa na dalili za karibuni za kambi yake, na upweke wa makazi yake (huyu kimada) yaliyotelekezwa, ukarimu na ushujaa (wa mwenye kimada), heshima isiyo na upinzani wa kabila lake, sifa nzuri za ngamia wake - hizi zilikuwa ndio mada ambazo, pamoja na tofauti ndogo katika utendaji, na bila hila yoyote ya njama au Hadith, zilitawala ndoto za Mwarabu - na baadhi ya hizo ziliongeza mafuta kwenye mazoea mabaya ya kudumu ya watu, makuu, uhasidi, kisasi na majivuno."
(The life of Mohammed, 1877)
Pamoja na kutokeza kwa Uislamu, msisitizo ulihamishwa kwa muda, kutoka ushairi kwenda nathari na ushairi ukapoteza nafasi yake ya ukubwa na hadhi kama vile "Malikia" wa sanaa za Arabuni. "Utungaji" mkubwa wa Uislamu ulikuwa ni Qura'n Tukufu, Kitabu cha Uislamu na kilikuwa katika nathari. Waislamu huamini kwamba Qur'an "iliandikwa" Mbinguni kabla ya kuteremshwa kwa Muhammad, Mjumbe wa Mungu.
Wanaamini kwamba kipaji cha mwanadamu kamwe hakiwezi kutoa kitu chochote ambacho kinaweza kulingana na mtindo wake au yaliyomo ndani yake. Kwa vizazi kumi na tano vilivyopita, imekuwa kwao mtindo wa maandishi, filosofia, theologia, sheria, metafisikia na mawazo ya kimafumbo.
Hii, inaonyesha kwamba Arabia kabla ya Uislamu ilikuwa haina vistawishi vya kijamii au historia ya kina, na Waarabu waliishi katika taflisi ya maadili na utumwa wa kiroho. Maisha kwao yalikuwa hayana maana, lengo na mwelekeo. Moyo wa ubinaadamu ulikuwa kwenye minyororo, na ulikuwa ukisubiri, kama ilivyokuwa, ishara ya kufanya jitihada kubwa mno, ya kujinasua na kuwa huru.
Ishara hiyo ilitolewa mwaka 610 A.D. na Muhammad, mwana wa Abdillah, katika mji wa Makka, alipotangaza ujumbe wake wa Utume, na akaanzisha harakati iliyoitwa Uslamu katika kazi yake ya kuzunguka dunia.
Uislamu ulikuwa ndio neema kubwa kwa mwanadamu daima uliwaweka huru wanaume na wanawake, kupitia utu kwa Muumba wao, kutokana na utumwa katika udhahiri wowote. Muhammad, Mtume (s.a.w.) wa Allah. (s.w.t.) alikuwa ndio mkombozi mkuu wa wanadamu. Yeye alimnasua mwanadamu kutoka kwenye "Mashimo ya Maisha"
Peninsula ya Arabia ki-jiogorafia ilikuwa pembezoni na kisiasa, eneo lisilojulikana mpaka mwanzoni mwa karne ya saba A.D. Ni wakati huo ambapo Muhammad (s.a.w.) alipoiweka kwenye ramani ya kisiasa ya dunia kwa kuifanya uwanja wa matukio ya maana sana ya historia.
Kabla ya Uislamu, Waarabu walishika nafasi ya pembeni tu katika historia ya Mashariki ya kati, na wangebaki daima taifa la watu wanaodhani kila kitu kina roho, na wachunga kondoo kama Muhammad (s.a.w.) asingewapatia kiini na kichocheo kilichoyaunganisha makabila yao ya kihamajihamaji yaliyokuwa yametawanyika, kwa nguvu yenye kujiendesha, yenye lengo maalum. Alitengeneza "taifa" kutoka kwenye bonge lenye mashimoshimo lisilokuwa na umbo la msingi. Aliwapamba Waarabu na nguvu mpya, udhanifu na kipaji cha ubunifu, na walibadili mwelekeo wa historia.
Alianzisha elimu ya viumbe na mazingira ya akili na falsafa mpya kabisa, na kazi yake iliweka kipindi cha waziwazi katika historia ya ulimwengu; na ilikuwa ni mwisho wa enzi moja na mwanzo wa nyigine.
Pamoja na kazi hii kubwa aliyoifanya Mtume wetu bado kuna watu ambao leo wanachukia kusoma na kupata elimu ya kimazingira na sayansi kwa madai kuwa ni ukafiri. Mfano wa makundi yenye watu wa aina hii ni Boko Haramu ya Nigeria ambali limeua watu wengi kwa kosa tu kwenda shule kusoma. Huu ni msiba kwa ulimwengu mzima wa kiislamu na ni harakati za wanafiki kuturudisha nyumba waislamu.

TOFAUTI ILIYOPO BAINA YA AHLU-SUNNA NA SHIA (ITHNA ASHARI).

Kuna tofauti baina ya Sunni na Shia katika masuala mbali mbali ingawa wote wanaunganishwa na kitu kimoja ambacho ni: Dini Tukufu ya Uislaam. Wote dini yao ni moja yaani Uislaam lakini tofauti ndogo zipo baina yao katika baadhi ya Masuala.
Tofauti kuu iliyopo baina ya Sunni na Shia ni hii ifuatayo:
Ahlu-sunna ambao hujulikana sana sana kwa walio wengi kama (Masunni) hufuata Makhalifa wanne (4) ambao wa kwanza wao ni Abu Abakar bin Kuhafa, na baada ya hao wanne hufuata Makhalifa wote wa Bani Umaiyya (yaani: Makhalifa wale wanaotokana na kizazi cha Bani Umaiyya).
Hivyo Ahlu-sunna wanafuata Makhalifa 4 wa mwanzo, wa kwanza wao akiwa Abu bakari na wa Mwisho wao akiwa Imam Ali (a.s), kisha baada ya hao wanafuata Makhalifa wote wa Banu Umaiyya, hata kama atakuwepo miongoni mwao Khalifa ambaye ni dhalimu, wao wanaamini ni wajibu kufuatwa dhalimu huyo na udhalimu wake sio sababu ya kutofuatwa, kwa ibara nyingine: Uadilifu wa Khalifa sio sharti la kukubalika kwake, bali anaweza kuwa Khalifa na ni wajibu kufuatwa hata kama atakuwa dhalimu na muovu.
Lakini Shia Ithna Ashari, wao ni wafuasi wa Maimam Maasumin Kumi na wawili (12) -a.s- kutoka katika Kizazi cha Mtukufu Mtume (s.a.w.w),hao ndio viongozi wao.
Hivyo Mashia hawaamini Makhalifa zaidi ya kumi na wawili (12) wala idadi pungufu ya kumi na mbili, maana hadithi ya Mtume (s.a.w.w) inasema Makhalifa baada yangu ni kumi na wawili(12), haisemi kuwa makhalifa baada yangu ni wanne (4) au zaidi ya 12.
Hivyo Mashia wanaona kwamba: Kuamini au kufuata Makhalifa wanne Abubakari, omar, Uthamn na Ali, ni kinyume na hadithi ya Mtume (s.a.w.w), maana hadithi hiyo haijasema kuwa Makhalifa ni wanne, bali imesema ni kumi na wawili(12), na akijitokeza mtu akasema: Sunni tunaamini Makhalifa wa kwanza wanne, kisha tunaamini ukhalifa wa makhalifa wa Banu Umaiyya, basi shia Ithna ashari hujibu kunako hilo kuwa kuwa: Makhalifa wa Banu Umaiyya idadi yao ilikuwa zaidi ya 12, wanafika 100 na zaidi, kwa hiyo hiyo nayo itakuwa ni kwenda kinyume na Hadithi ya Mtume (s.a.w.w) kuwa Makhalifa baada yake ni kumi na wawili (12), kwa maana kwamba;Makhalifa hawatakiwi kupungua wala kuongezeka katika idadi hiyo iliyotajwa na Mtume (s.a.w.w) katika hadithi sahihi iliyopokelewa na madhehebu zote za kiislaam.
Hii ndio tofauti kuu inayopatikana baina ya Shia Ithna Ashari na Ahlu-sunna. Kunako tofauti hii unaweza kurejea kitabu kiitwacho:
Tarikh Al-madhahibul-Islamiyya: Juzuu ya 2; ukurasa wa 11-12

HASHIM - KABLA YA KUZALIWA UISLAMU sehemu ya kwanza

Katika karne ya tano (A.D). mtu aliyeitwa Qusay, alizaliwa katika kabila la Quraish. Alipatia heshima kubwa na umaarufu kwa kabila lake kwa ajili ya hekima zake. Aliijenga upya Al-Kaaba iliyokuwa katika hali ya kukatisha tamaa, na aliwaamuru Waarabu kujenga nyumba zao kuizunguka. Alijenga pia "ukumbi wa mji" wa Makka, wa kwanza katika Arabia. Viongozi wa koo mbalimbali walikusanyika katika ukumbi huu kutafakari juu ya maswala yao ya kijamii, kibiashara, kiutamaduni na kisiasa. Qusay aliunda sheria juu ya kugawa chakula na maji kwa Mahujaji waliokuja Makka, na aliwashawishi Waarabu kulipa kodi kwa ajili ya msaada wa huduma zao.
Edward Gibbon anasema:
"Qusay, aliyezaliwa takriban A.D. 400, ni babu yake mkubwa Abdul-Muttalib, na hivyo wa tano katika kizazi cha kupanda toka Muhammad, alipata mamlaka makubwa huko Makka.
(The decline and Fall of the Roman Empire)
Qusay alifariki mwaka 480 A.D., na mwanae, Abd Manaf, alitwaa madaraka ya kazi zake. Na yeye pia alijipatia sifa kutokana na uwezo wake. Alitambulika kwa ukarimu wake na maamuzi yake mazuri. Alifuatiwa na mwanae Hashim. Ni huyu Hashim aliyeupa ukoo wake jina lake uliokuja kuwa maarufu katika historia kama Bani Hashim. Hashim alikuwa ni mtu wa namna ya pekee. Alikuwa ni yeye aliyewafanya Maquraishi kuwa wafanyabiashara na wakawa wafanyabiashara bora. Alikuwa ndiye mtu wa kwanza kuanzisha zile safari mbili za misafara ya Maquraish, ya kiangazi na kipupwe, bila yeye, Waarabu wangeweza kubakia wachunga kondoo daima.

HASHIM - KABLA YA KUZALIWA UISLAMU sehemu ya pili

Uongozi wa uongofu na wema na ukarimu zilikuwa ni mbili tu kati ya sifa nyingi ambazo Muhammad, nabii wa baadaye, "alizorithi" toka kwa mababu zake. Hashim alioa mwanamke wa Yathrib na kutokana naye alipata mtoto wa kiume - Abdul-Muttalib. Kwa wakati upasao, Abdul Muttalib alikuwa amrithi baba yake kama mkuu wa ukoo wa Hashim.
Edward Gibbon:
"Huyu babu yake Muhammad (Abdul Muttalib), na nasaba yake ya jadi, wanaonekana katika kumbukumbu za kigeni na za ndani kama mabwana (wafalme) wa nchi yao; lakini walitawala, kama Percales huko Athens, au Medics huko Florence, kwa maoni ya hekima zao na msimamo; athari zao ziligawanyika pamoja na urithi wao. Kabila la Kuraish walijipatia usimamizi wa Al-Kaaba; ile ofisi ya kikasisi iliyoendelezwa kupitia mishuko minne ya nasaba hadi kwa babu yake Muhammad; na ukoo wa Hashim, kutoka pale alipochipukia, lilikuwa ndio liliheshimiwa sana na tukufu kwenye macho ya nchi yao.
Mshuko wa Muhammad kutoka kwa Ismail ulikuwa ni hadhi ya taifa au hekaya, lakini kama hatua za mwanzo za jadi hii ni za giza na mashaka angeweza kutoa vizazi vingi vya uungwana (usharifu) safi na halisi; alichipukia kutoka kwenye kabila ya Quraish na ukoo wa Hashim ulio maarufu sana wa Waarabu, mabwana wa Makka, wasimamizi warithi wa Al-Kaaba.
(The Decline and Fall of the Roman Empire)
Hashim alikuwa na ndugu yake mdogo alikuwa akiitwa Al-Muttalib, mtoto wa Abd Manafi. Kwa kipindi, alikuwa ndiye mkuu wa ukoo huo, na alipofariki mpawe - Abdul Muttalib - mtoto wa Hashim, alimfuatia yeye kama mkuu mpya wa ukoo huo. Abdul Muttalib alidhihirisha sifa zote zilizoyafanya majina ya baba na babu yake kuwa makubwa na maarufu.
Kama ilivyoonekana kabla, mji wa Makka kama Arabia yote, ulikuwa hauna serikali wala mtawala, lakini ulimilikiwa na kabila la Quraish. Quraish ilitokana na koo kumi na mbili, na Banu Hashim ulikuwa mmoja wao. Kwa kupinga uharibifu wa tabia wa nyakati; watu wa ukoo wa Banu Hashim, walikumbuka, nusu karne kabla ya kuzaliwa Muhammad, kufanya juhudi za kujaribu kuzuia kuanguka kwa maadili ya Waarabu na kuimarisha hali ya kijamii, kiuchumi na ukuzi wa akili ya nchi hiyo. Wao, kwa hiyo, walibuni au kuunda shirikisho la wenye maadili. Malengo makuu ya shirikisho yalikuwa kuzuia vita kutokana na kugawanyika na kuwalinda wanyonge na wasio na ulinzi kutoka kwa maadui.
Hawa Banu Hashim vilevile walijishughulisha katika ustawi wa uchumi wa Waarabu na walianzisha mfumo wa biashara na nchi majirani kwa kutuma misafara kwenda Syria wakati wa kiangazi na Yemen wakati wa kipupwe, kama ilivyoelezwa kabla. Misafara iliondoka Makka ikiwa imebebeshwa bidhaa kama matunda ya tende, lijamu na hatamu za farasi na ngamia, mablanketi yaliyotengenezwa kwa sufi au manyoya ya ngamia; manukato na mimea yenye kunukia uzuri, viungo, ubani, pembe na ngozi za wanyama wa jangwani, na farasi wa ukoo safu. Walirudi na nguo, mafuta ya zeituni, silaha, kahawa, matunda na nafaka.
Yote haya, shirikisho la wenye maadili na biashara ya misafara yalikuwa, bila ya ubishi, ni zawadi kubwa ya Bani Hashim kwa Waarabu. Lakini zawadi kubwa mno sio tu kwa Waarabu, bali kwa dunia nzima, ilikuwa iwe ni yule mtoto aliyekuwa aitwe Muhammad mwana wa Abdullah ibn Abdul Muttalib na Amina binti Wahab, alikuwa aje kuwa mfadhili mkuu, sio tu kwa Waarabu bali kwa wanadamu wote. Moja ya matukio maarufu lilitokea wakati wa wajibu wa Abdul Muttalib kama msimamizi wa Al-Kaaba, lilikuwa ni uvamizi wa Makka toka kwa jeshi la Kihabeshi likiongozwa na yule jemadari wa Kikristo, Abraha. Hilo jaribio la kuiteka Makka lilishindwa kama ilivyoelezwa katika Aya ya Qur'an Tukufu ifuatayo:
"...Na akawapelekea juu yao, ndege makundi makundi, wakawatupia mawe ya udongo mkavu. Na akawafanya kama majani yaliyotafunwa tafunwa." (Sura ya 105: 3-5 )
Kawa vile wavamizi walikuja na tembo (ndovu), ule mwaka wa kampeini yao ulikuja kujulikana kama "Mwaka wa Tembo". Huu mwaka wa Tembo uko sawia na mwaka 570 A.D. ambao pia umetokea kuwa ndio mwaka wa kuzaliwa Muhammad, nabii wa wakati ujao. Lile jeshi la uvamizi liliondoka Makka, na masharti ya makubaliano ya kusimamisha vita yakajadiliwa, kwa niaba ya mji wa Makka, na Abdul Muttalib.
Sir John Glubb:
"Mnamo mwaka 570 A.D. Abraha, kaimu mfalme wa Kikristo wa Uhabeshi wa huko Yemen aliingia Makka. Makuraish walikuwa waoga sana au wanyonge mno wa kulipinga jeshi hilo la Kihabeshi na Abdul Muttalib, akiongoza ujumbe, alitoka kwenda kujadiliana na Abraha.

KUZALIWA KWA MUHAMMAD (S.A.W.W) NA MIAKA YA MWANZO YA UHAI WAKE

KUZALIWA KWA MUHAMMAD (S.A.W.W) NA MIAKA YA MWANZO YA UHAI WAKE
Abdullah alikuwa ndiye mtoto kipenzi cha Abdul Muttalib.
Alipokuwa na umri wa miaka kumi na saba, alimuoa Amina, bibi wa uzao bora wa Yathrib, mji ulioko Kaskazini ya Makka. Hakuwa hata hivyo, amekadiriwa kuishi muda mrefu, na akafa miezi saba tu baada ya ndoa yake.
Muhammad, Mtume wa Mungu wa wakati ujao, alikuwa bado mimbani. Sheikh Muhammad el-Khidhri Buck, profesa wa historia ya Kiislamu, chuo kikuu cha Misri, Cairo, anasema katika kitabu chake, Nur-ul-Yaqin fi-sirat Sayyid al-Murasalin (1953) hivi:
"Yeye (Muhammad Ibn Abdullah) alizaliwa katika nyumba ya ami yake, Abu Talib, katika "mtaa wa Bani Hashim" huko Makka, tarehe 12 Rabil-awal y ule Mwaka wa Tembo, tarehe ambayo inaoana na tarehe 8 Juni 570. Mkunga wake alikuwa ni mama yake Abdur Rahmani Ibn Auf. Mama yake, Amina, alituma habari za uzazi huu wa kheri kwa babu yake, Abdul Muttalib, ambaye alikuja, akamchukuwa mikononi mwake, na akampa jina hili la Muhammad."
Mgao wa Muhammad katika urithi wake ulikuwa ni mtumwa mmoja wa kike, Ummu Ayman; ngamia watano na kondoo kumi. Huu ni ushahidi kwamba Mitume wanaweza kurithi mali, na kama wanaweza kurithi mali toka kwa wazazi wao, wanaweza pia kurithisha mali kwa watoto wao wenyewe. Kuwa mitume hakuwabatilishii wao katika kupokea urithi wao wenyewe wala hakuwabatilishii watoto wao kupokea wa kwao. Kauli hii inaweza kuonekana kama isiyofuata mantiki katika muktadha huu lakini sio. Muhammad, Mtume wa Uislamu, alitoa kwa mwanae, Fatima kama zawadi, shamba la Fadak.
Lakini alipofariki; Abu Bakr, aliyekuwa Khalifa, na Umar, Mshauri wake, walilikamata shamba hilo kwa kisingizio kwamba Mitume hawarithishi mali yoyote kwa watoto wao wenyewe, na mali yeyote wanayomiliki, inahusika baada ya kifo chao, sio kwa watoto wao, bali kwa umma wao. Ni faini kali ambayo mtu anapaswa kulipa katika Uislamu kwa kuwa tu mtoto au binti wa Mtume wake. Mtu mwingine yeyote katika umma huu anayo haki ya kurithi utajiri au mali ya baba yake lakini sio binti wa Muhammad, Mtume wa Allah (s.w.t.)!

MASHIA NI WATEKELEZAJI WA AMRI ZA MTUME MOHAMMAD (S.A.W.W)

Mashia wanatekeleza amri ya Mtume (s.a.w.w) inayosema: "Nimekuachieni vizito viwili, Kitabu cha Mwenyezi Mungu na Kizazi changu, vitu ambavyo mkishikamana navyo kamwe hamtapotea baada yangu." Kama ambavyo zinashuhudia Sihah za Sunni ukiachilia mbali vitabu vya Kishia.
Badala ya kuwashukuru (Mashia) na kuwatanguliza na kuwaboresha juu ya wengine kwa kufuata kwao maamrisho ya Mtume (s.a.w.w.), tunawashutumu na kuwakufurisha na kujitenga nao, jambo hili siyo uadilifu wala haliingii akilini.
Mimi na mashia wote tunapinga kauli za kijinga na za uongo ambazo haziwezi kusimamisha dalili wala hoja na hazina uzito kwa wanataaluma miongoni mwa watoto wa umma wetu kwamba, "Eti Mashia wanayo Qur'ani yao, au eti wao wanasema kwamba aliyepewa Utume ni Ali, au kwamba Abdallah ibn Sabaa' Myahudi ndiye muanzilishi wa Ushia."Na mengineyo miongoni mwa kauli dhaifu ambazo Mwenyezi Mungu anashuhudia kuwa hayo ni miongoni mwa uzushi wa maadui wa Uislamu na maadui wa Ahlul-Bait na wafuasi wao. Na hayo ni mambo hayakuzushwa isipokuwa ni kutokana na ubinafsi mpotovu na ujinga wenye kero iliyopita kipimo

MIAKA YA MWANZO YA MTUME MOHAMMAD (S.A.W.W)

Ilikuwa ni desturi miongoni mwa Maquraish kuwapeleka watoto wao jangwani kupitisha miaka yao ya mwanzo katika hali ya hewa ambayo ilikuwa ni yenye kutia afya kuliko ile ya Makka. Watoto walijenga miili yenye nguvu zaidi katika maeneo ya wazi na hewa safi ya jangwani kuliko ambavyo wangekuwa katika hewa ya mjini yenye kusonga na kukirihi.
Kulikuwa na sababu nyingine moja zaidi ya kwanini Waarabu wa koo bora waliwapeleka watoto wao kuishi jangwani. Walikuwa wanasisitiza ufasaha katika kuongea na walikuwa "washabiki" wakubwa wa maneno. Walivutiwa na lugha ya Kiarabu, maneno yake, maana zao na tofauti ndogo ndogo katika maana zao; na walijivunia sana katika ufasaha wao binafsi. Kwa kweli, matabaka ya juu katika Makka walipata mamlaka yao juu ya uwezo wao wa balagha. Makka ilikuwa ndio sehemu ya makutano ya misafara mingi na Kiarabu chake kilikuwa kimechafuliwa na kuwa "Kiarabu pijini" (chenye maneno mchanganyiko).
Waarabu wa koo bora hawakutaka watoto wao kujifunza na kuongea kiarabu pijini cha Makka; waliwataka wazungumze tu lugha safi na isiyochanganywa ya jangwani. Wao, kwa hiyo, waliwapeleka watoto wao mbali na Makka ili kuwakinga kutokana na athari zote haribifu kama hizi katika miaka yao ya awali ya maisha yao.
Amina alimtoa mwanae, Muhammad, kwa Halima, mwanamke wa kabila la Banu Asad, aliyekuwa akiishi Mashariki ya Makka, kwa ajili ya malezi. Mtoto mchanga huyu, Muhammad aliishi miaka yake minne ya kwanza ya maisha yake huko jangwani na mama mnyonyeshaji wake. Wakati fulani katika mwaka wake wa tano wa maisha yake, mama huyu anasemekana alimrudisha kwa mama yake huko Makka.
Muhammad alikuwa na umri wa miaka sita wakati Amina, mama yake, alipofariki. Alichukuliwa baadae na Abdul Muttalib, babu yake, mpaka nyumbani kwake. Lakini miaka miwili tu ilipita wakati Abdul Muttalib naye alipofariki.

HISTORIA YA MADHEHEBU YA AHLU-SUNNA, MWANZO WAKE NA CHIMBUKO LAKE:

HISTORIA YA MADHEHEBU YA AHLU-SUNNA, MWANZO WAKE NA CHIMBUKO LAKE:
Maulamaa na wanazuoni wa Kisunni wametofautiana kuhusiana na chimbuko la madh-hebu hii ya Ahlu-sunna, kwamba ni lini hasa ilianza madh-hebu hii au ni nani haswa mwasisi wake?!. Zimekuwapo fikra na rai mbali mbali kwa wanazuoni hao kunako hilo.Tunazitaja kama ifuatavyo:
1- Baadhi yao wamesema kwamba: Chimbuko la Madh-habu hii lilikuwa ni katika zama za uhai wa Mtume (s.a.w.w), na kwamba Muasisi wa Madh-hebu hii ni Mtume mwenyewe (s.a.w.w). Kwa mujibu wa rai hii, ina maana madhehebu zote zilizobaki (tofauti na madh-hebu ya Ahlu-sunna) hazikuwepo zama za Mtume (s.a.w.w), hivyo zitakuwa ni Madh-hebu zilizokwenda kinyume na kupotea na hazina itibari yoyote. Kunako rai hii unaweza kurejea kitabu kiitwacho:
{Itiqadi Ahlu-sunna As-habul-Hadithi, ukurasa wa 11}.
2- Wakasema wanazuoni wengine (hao hao wa kisunni) kuwa: Fikra na Rai ya kwanza sio sahihi kuhusu chimbuko la Ahlu-sunna, bali ukweli ni kwamba: Madh-hebu hii ya Ahlu-sunna chimbuko lake ni siku ile aliyofariki Mtume Muhammad (s.a.w.w) ambapo kundi kubwa la waislaam (Maswahaba) waliungana na Abubakar bin Kuhafa na kumchagua kuwa Khalifa, na kundi lingine la pili la maswahaba likaungana na Imam Ali bin Abiu Twalib (a.s) na watoto wake Imam Ali (a.s), nalo ni kundi lile ambalo halikwenda katika ukumbi wa Saqifa kuchagua nani atakuwa Khalifa baada ya Mtume (s.a.w.w) bali kundi hili lilibakia nyumbani kwa Mtume (s.a.w.w) likiwa pamoja na Imam Ali bin Abi Talib (a.s) kwa ajili ya shughuli nzima ya kuuosha mwili Mtukufu wa Mtume (s.a.w.w), kuuvalisha sanda, na maandalizi yote kwa ujumla ya kimazishi.
Hao ndio waliokataa Ukhalifa wa Abubakar na kusema hasitahiki kuwa Khalifa isipokuwa Imam Ali bin Abi talib (a.s) maana huyu ndiye aliyeteuliwa na Mtume (s.a.w.w) na wakasema Khalifa hachaguliwi na waislaam bali anachaguliwa na Mwenyeezi Mungu (s.w) kupitia kwa Mtume wake (s.a.w.w). Wakapinga uchaguzi huo wa ukhalifa kwa Abubakar na kusema si jukumu la waislaam kuchagua Khalifa maana Mtume tayari kaisha teua khalifa baada yake na huyo ndiye tunayetakiwa kumfuata na kurejea kwake baada ya Mtume (s.a.w.w).
Hivyo Masahaba wakagawanyika makundi pande mbili, wanaokubali ukhalifa wa Abubakar kuwa ndio khalifa maana watu wamemchagua, na upande mwingine wa maswahaba ukawa kwa Imam Ali (a.s) na kuthibitisha ukhalifa wake ukisema upande huu kuwa: Khalifa ni yule tu aliyechaguliwa na Mtume (s.a.w.w) katika uhai naye ni Imam Ali bin Abi Talib (a.s). Tangu hapo ndipo likachimbuka jina la Ahlusunna na Shia, kwamba:
Wale Maswahaba waliokuwa upande wa Abubakar na kumchukulia kuwa yeye ndiye Khalifa walijulikakana rasmi kama {Ahlu-sunna} na wale Masahaba waliokuwa upande wa Imam Ali bin Abi Twalib (a.s) wakifuata hadithi za Mtume (s.a.w.w) za kumteua Ali kuwa wasii wake na khalifa baada yake, wakajulikana kama {Mashia au wafuasi wa Ali bin Abi Talib (a.s). Kuhusu rai hii unaweza kurejea katika kitabu kiitwacho:
(Min Hayat Al-khalifatu Abi bakari, cha Allama, Sheikh Abdul-Hasani Al-amini, ukurasa wa 30).
3- Rai ya tatu ya wanazuoni wa kisunni kunako chimbuko la Ahlu-sunna inasema:
Madh-hebu ya Ahlu-sunna chimbuko lake si katika zama za uhai wa Mtume (s.a.w.w) na wala sio siku ile aliyofariki Mtume Muhammad (s.a.w.w), bali ukweli halisi ni huu kwamba: Madh-hebu hii imeasisiwa baada ya kifo cha Mtume (s.a.w.w), na kwamba Mtume (s.a.w.w) hajaacha kitu kinachoitwa Ahlu-sunna wal-jamaa, bali istilahi hiyo ya Ahlusunna imezuka au imeasisiwa au imechimbuka katika zama za Ukhalifa wa Muawia bin Abi Sufiyani, yeye (yaani Muawia) ndiye mwanzilishi wa neno hili Ahlu-Sunna, na alianzisha neno hilo au istilahi hiyo pale alipofanya sulhu na Imam Hasan bin Ali bin Abi Talib (a.s) ambapo baada ya sulhu iliyojiri baina ya Imam Hasan (a.s) na Muawia, alisimama Muawia na kutangaza akisema: Hii ni Sulhu ya Ahlu-sunna Wal-jamaa, nayo ni ile Suhlu iliyofanyika baina ya Masunni hao na wafuasi wa Ahlu-bait (a.s) ambao wakati wa zama hizo za Muawia walikuwa wakimtawalisha Imam Hasan (a.s) na kuthibitisha kuwa yeye ndiye Khalifa wa Pili baada ya Imam Ali bin Abi Talib (a.s).
N/B: Rai ya hii ndio rai yenye uzito zaidi maana ndio inayothibitisha kiusahihi chimbuko au mwanzilishi wa Istilahi hii ya Ahlu-sunna. Hivyo Istilahi haikuwepo zama za uhai wa Mtume (s.a.w.w) na hata baada ya Kifo cha Mtume (s.a.w.w) haikuwepo mpaka pale Muawia alipokuwa Khalifa ndio akaja na Istilahi hii ya Ahlu-sunna wal-jamaa katika tukio hilo tulilolitaja sehemu hii (ya sulhu).
Kunako rai hii unaweza kurejea kitabu kiitwacho:
As-saqifa Ummul-Fitna, cha Jawad bin Jaafar Al-khalili, ukurasa wa 17.
4- Rai ya nne na ya mwisho inayotolewa na wanazuoni wa kisunni inasema hivi:
Madhehebu ya Ahlu-sunna imepatikana kutokana na juhudi za maulamaa wakubwa wa Ahlu-sunna (yaani: Maulamaa wakubwa wa Kisunni) kama vile: ABU HANIFA, MALIK BIN ANAS, IMAM SHAFI, HANBALI, ABU MUSA AL-ASH-ARI na wengine.

USHUHUDA WANGU JUU YA SHIA WA AHLULBAYT (a.s)

Hapo zamani nilikuwa Muwahhabi kama ninyi nimefunikwa sioni haki wala Ahlul-Bait (a.s.) na wafuasi wao. Mwenyezi Mungu akaniongoza kuelekea kwenye haki ambayo hapana baada yake ila upotovu, na nikawa huru kutokana na minyororo ya ung'ang'anizi na kufuata kama kipofu, na nilifahamu kwamba wengi wa Waislamu bado wamefunikwa na habari zisizo na ukweli na za uzushi. Kampeni zilizoandaliwa kuwapa baadhi ya watu utukufu wasiostahili zinawazuwia (Waislamu) kuufikia ukweli ili wote wapate kupanda meli ya uokovu na washikamane na kamba imara ya Mwenyezi Mungu, na hakuna tofauti kama mjuavyo baina ya Sunni na Shia isipokuwa ni katika yale waliyotofautiana kwa ajili ya Ukhalifa baada ya Mtume, na msingi wa tofauti ni itikadi yao kuhusu Masahaba, nao Masahaba (r.a.) walitofautiana kati yao mpaka wakalaaniana, kupigana na kuuana wao kwa wao. Ikiwa kutofautiana kati yao ni kutoka katika Uislamu basi Masahaba ndiyo wa mwanzo kutuhumiwa kwa tuhuma hii na Mwenyezi Mungu apishe mbali.
Mimi nilistaajabia uadilifu wa wapinzani wa ushia kwani kama ambavyo Mashia wana desturi ya kuwatukuza Ahlul-Bait (a.s.) na kuwaheshimu vile vile Masunni wanayo desturi ya kuwatukuza Masahaba wote, na misimamo hii miwili iko mbali mbali. Kwa nini Shia wakufurishwe kwa kuwaheshimu Mtume na Ahlulbayt wake? Lakini wanaowatukuza Maswahaba wote kwa umoja wao waonekane ndio waislamu sahihi?
Basi ikiwa Mashia kwa desturi yao hiyo wanakosea, basi Masunni ndiyo watakaokuwa wanakosea zaidi (katika desturi yao) kwani Masahaba wote wanawatanguliza Ahlul-Bait (a.s.) kuliko nafsi zao, na huwatakia rehma kama wamtakiavyo rehma Mtume (s.a.w.w.). Na hatumfahamu yeyote miongoni mwa Masahaba (r.a.) aliyeitanguliza nafsi yake au aliyejitukuza juu ya watu wa nyumba ya Mtume (s.a.w.w.) katika elimu au matendo mema.

UTAFITI ULIONIFANYA NIWE MSHIA ITHNAASHARIYYAH

Ilikuwa kutafuta utaratibu na fikra iliyowiva na taaluma itakiwayo ni vigumu, na daraja hii
ilikuwa chungu, japokuwa utafiti wangu ulikuwa kwa sura ya msamaha na wa kimaumbile.
Katika maisha yangu ya kawaida nilikuwa nauliza na kujadili na vinginevyo, wala hapakuwa na utayarifu wa kutafiti na kuhimili. Na baada ya uvamizi mkali wa mawahabi kuivamia Sudan, na kushika kasi malumbano na mijadala na kukithiri kwa harakati za kidini, ukweli mwingi ulifichuka, na zikajitokeza tofauti na mifarakano mingi ya kihistoria, kiitikadi na kifiq’hi.
Na tendo la kuvikufurisha baadhi ya vikundi na kuvitoa nje ya tanzi la uislamu ilianza, ni
miongoni mwa mambo ambayo yalisababisha mfarakano wa kimadhehebu na safu
kutengana. Pamoja na uchungu wa yaliyotokea, nilipata utashi wangu na udadisi wangu
ulizidi, na nilikuwa naona uhalisi wa yale maswali yaliyokuwa yanaishawishi akili yangu.
Hapo basi hima yangu ya kuutilia maanani uwahabi ilizidi, nilikuwa nafuatilia mijadala yao na mikusanyiko yao ambayo ilikuwa inanifunga mimi. Na ambalo ni la muhimu nililojifunza kutoka kwao katika ngazi ile, ni ujasiri na kuukabili ukweli na kuukinza, nami nilikuwa naamini kuwa ukweli ni kitu kitakatifu na ni mwiko kuuhujumu au kuupinga, japokuwa uangalizi wangu ulikuwa mwingi kuuhusu, ambapo aghlabu nilikuwa siangalii kupitia dhati yangu na umbile langu, hivyo basi nilikuwa najizuia sana matendo na zoezi za jamii ya kidini.
Niliendelea nao, na ilijiri kati yangu na wao mijadala mingi, ambayo ukweli wake ulikuwa
yale maswali ambayo yalikanganya akili yangu, baadhi yake nilipata majibu yaliyoniridhisha katika ngazi ile, na kulikuwa na maswali sikupata majibu yake kutoka kwao, hilo lilikuwa dhamana tosha kwangu kuwaelemea na niwaunge mkono, japokuwa kulibaki baadhi ya mazingatio ambayo yalikuwa kizuizi kati yangu na kujihusisha moja kwa moja na mwendo wa kiwahabi.
La kwanza na la muhimu ni kuwa mimi sikupata kwao nitoshekalo nalo,
ambalo laweza kuwa jibu la matamanio yangu ya kiujumbe. Na wakati mwingine wasiwasi ulikuwa unanichukua kwa kauli yake: Kwa kweli unalolifikiria na kulitafiti ni kitu cha mfano tu hakina ukweli, na uwahabi ni sampuli bora ya uislamu na hapana kitu badala yake….
Nilikuwa nasukumwa na wasiwasi huu na kuusadiki kwa kutokuwa kwangu na maarifa na fikra za vyuo vingine, lakini haraka nilikuwa nang’amua kuwa ambalo Jamaludin amelifanya haiwezekani liwe ndio hii fikra ya kiwahabi. Kwa hiyo nilikuwa nasema waziwazi: Kwa kweli Uwahabi ni njia ilio karibu mno kuelekea Uislam, kwa sababu yale wayafanyayo kuonyesha dalili, na matamko rasmi ya kisheria ili kuthibitisha ukweli wa madhehebu yao, ni jambo ambalo sijaliona katika vikundi vingine humu (nchini) Sudan.
Lakini tatizo lao ni kuwa madhehebu hii waliojijengea yashabihiana mno na kanuni za
hisabati, kwani yenyewe ni desturi na kanuni iliyoganda, hutekelezwa bila ya kuwa na akisi ya kimaendeleo iliyo wazi katika maisha ya mwanadamu. Na katika fani ya kuamiliana na dunia hii katika nyanja tofauti za mtu mmoja au za kijamii au ya kiuchumi au kisiasa… na hata jinsi ya uhusiano na Mwenyezi Mungu (s.w.t).
Bali ni kinyume kabisa mara nyingi humfanya mtu awe mkiwa mwenye kujitenga mbali na jamii, kwa aliyonayo miongoni mwa ufinyu wa fikra katika kila mikato yake. Mtu miongoni mwao hawezi kuishi na jamii bali huwa ni mwenye kujipambanua mbali nao kwa vazi lake na mwenendo wake na katika kila sehemu ya maisha yake, na hata jinsi ya uongeaji wake, hazoeani ila na watu wa aina yake.
Nilikuwa nahisi kuwa wameghurika na wenye kiburi na dharau kwa kuwa wao huwaangalia watu wengine wakijiona wao wako juu, hawana maingiliano nao wala hawashirikiani nao katika maisha yao.
Vipi watashirikiana nao?! Hali kila lifanywalo na jamii ya kiislamu kwao ni bidaa na
upotovu. Mimi nakumbuka vyema ulipoingia mvuto wa kiwahabi kijijini petu katika muda
mfupi na bila ya darasa lolote wala uelewa, kundi kubwa la vijana walijiunga kwenye
uwahabi, hawakuendelea muda mwingi wote walijitoa, na hili lilikuwa ndio tazamio langu,
kwa sababu madhehebu mpya imewazuia kuchanganyika na jamii na iliwaharamishia
kawaida nyingi ambazo walilelewa nazo, hali zikiwa haziendi kinyume na dini.
Na jipya nikumbukalo ni kuwa, miongoni mwa vitu ambavyo vijana waliojiunga na uwahabi walikuwa wanataabika navyo, ni kwamba ilikuwa ni kawaida kijijini petu vijana zama za usiku wa mbaramwezi hujumuika na kuketi kwenye mchanga ulio safi wanapitisha wakati wao huko, nao ni wakati pekee wa kuonana vijana wa kijijini ambao wanafanya kazi mchana kutwa katika mashamba yao na katika shughuli zao walizozizoea, basi Sheikh wao alikuwa anawazuia kufanya hivyo na kuwaharamishia tendo hilo kwa hoja ya kuwa Mtume wa Mwenyezi Mungu (s.a.w.w) ameharamisha kukaa njiani, japokuwa sehemu hizi hazizingatiwi kuwa ni njia

KUTOFAUTIANA KATI YA SHIA NA WAISLAMU WENGINE KULIANZA LINI?

Hitilafu baina ya Shia na Waislamu wengine wasio Shia haikuanza juzi na jana. llianza karne nyingi zilizopita; mara tu baada ya Mtume Muhammad s.a.w.w. kufariki dunia. Hata hivyo, katika kipindi cha Makhalifa wawili wa kwanza, hitilafu hiyo haikuzusha zogo na fitina kubwa kama lile lililozuka katika kipindi cha Makhalifa wa tatu na wa nne.
Baada ya Khalifa wa tatu (Khalifa Uthman) kuuliwa, na mtu aliyekiitwa Muawiya kuongoza upinzani dhidi ya Khalifa wa nne (Imam Ali), ndipo hitilafu hiyo ilipopaliliwa moto. Na kutokana na upinzani huo ndipo Imam Ali a.s. alipolaaniwa, kwa amri ya Muawiya, katika hotuba zote za Ijumaa, kwa muda usiopungua miaka themanini. Ndipo wote wale waliokimtambua Imam Ali a.s. kuwa ni imamu wa haki (yaani Shia) walipokuwa wakisakwa kama nyoka na kuuawa! Ndipo Imam Hassan a.s., mjukuu wa Mtume s.a.w.w., alipouliwa kwa kutiliwa sumu chakulani mwake! Ndipo Imam Hussein a.s., mjukuu mwingine wa Mtume s.a.w.w., alipouliwa kinyama huko Karbalaa (lraq) kwa kukatwa kichwa chake, Kikatungikwa kwenye mkuki na kuchezewa ngoma, na kuliacha pingiti la mwili wake lishetwe-shetwe na farasi! Ndipo hofu ilipofikia kiwango cha watu, chini ya Ufalme wa Muawiya, kuogopa kuwapa watoto walio wazaa jina la Ali! Ndipo hata mashekhe, kwa kuchelea kuadhibiwa na kuuawa, walipokiogopa kulitaja jina la Imam Ali a.s. katika riwaya za Hadith za Mtume s.a.w.w.; badala yake ikawa husema: 'Amesema Sheikh'!

MOHAMMAD (S.A.W.W) AITWA MKWELI MWAMINIFU

MOHAMMAD (S.A.W.W) AITWA MKWELI MWAMINIFU
Mapema katika maisha, Muhammad, nabii alijenga sifa ya ukweli, uaminifu na maamuzi yenye busara. Kwa vile hakukuwa na mabenki siku zile, alikuja kuwa "benki" ya watu wa Makka. Walileta fedha zao, mapambo ya vito, na vitu vinginevyo vya thamani kwake kwa uhifadhi wa salama, na wakati wowote walipotaka kurudishiwa kitu chochote, aliwarudishia. Walimuita yeye al-Amin (Mwaminifu) na as-Sadiq (Mkweli).
"Kwa kujaaliwa na akili safi adilifu na tamaa dhaifu, mkimya na mwenye mazingatio, yeye (Muhammad) aliishi zaidi kiupweke, na tafakari ya moyoni mwake ilimpatia shughuli kwa masaa ya mapumziko yaliyotumiwa na watu wenye tabia duni katika michezo ya kikatili na ufisadi. Tabia njema na muelekeo wa heshima wa kijana huyu asiyejionyesha vilimletea kukubalika kwa wananchi wenzie; na alipata lile jina, kwa kuafikiana kwa jumla, la Al-Amin, 'mwaminifu.' Hivyo aliheshimiwa na kutukuzwa, Muhammad aliishi maisha ya utulivu na ya kitawa katika familia ya Abu Talib." (The life of Muhammad 1887, uk 20).

WAULIZENI WENYE KUMBUKUMBU IKIWA NINYI HAMJUI (QUR. 16:43 NA 21:7)

WAULIZENI WENYE KUMBUKUMBU IKIWA NINYI HAMJUI (QUR. 16:43 NA 21:7)
Bila shaka aya hii Tukufu inawaamuru Waislamu kuwarejea watu wenye kumbukumbu kwa kila linalowatatiza ili wapate kuufahamu muelekeo ulio sawa, kwani Mwenyezi Mungu amewaandaa (wenye kumbukumbu) kwa ajili hiyo baada ya kuwafunza, basi wao ndiyo waliobobea katika elimu na ndiyo wanaofahamu Ta'wili ya Qur'an.
Kwa hakika aya hii ilishuka kuwatambulisha Ahlul-Bait (a.s.) nao ni Mtume Muhammad, Ali, Fatma, Hasan na Husein, na hili lilitendeka katika zama za Mtume. Amma baada ya Mtume (s.a.w.w.) mpaka kitakaposimama Qiyama (wenye kumbukumbu) ni hawa hawa watano waliotajwa ambao ndiyo Ahlul-Kisaa na huongezwa kwa hao, Maimamu tisa kutoka katika kizazi cha Hussein (a.s.) ambao Mtume wa Mwenyezi Mungu amewabainisha katika Minasaba mbali mbali na akawaita kuwa ni Maimamu wa uongofu na ni taa ziondoazo kiza na wao ndiyo wenye kumbukumbu, na ndiyo waliobobea katika elimu, Mwenyezi Mungu amewarithisha elimu ya kitabu.
Riwaya hizi zimethibiti na ni sahihi tena mutawatir kwa Mashia tangu zama za Mtume (s.a.w.w.), na wamezieleza baadhi ya wanachuoni wa Kisunni, na wafasiri wao wamekiri kwamba kushuka kwa aya hii kunawahusu Ahlul-Bait (a.s.). Ninawataja miongoni mwa wanachuoni hawa kwa kutolea mfano:
1) Im1)Imam Thaa'labi katika Tafsiri yake (alipozunhumzia) maana ya aya hii katika Surat An-NahliNahl.
3) Tafsirul-Qur'an ya ibn Kathir Juzuu ya pili ukurasa 570570.
3) Tafsirut-Tabari, Juzuu ya kurni na nne ukurasa 109.
4) Tasirul-Alusi iitwoyo Ruhul-Maani Juzuu ya kumi na nne ukurasa wa 134.
5) Tafsirul-Qurtubi Juzuu ya kumi na moja ukurasa 272.
6) Tafsirul-Hakim iitwayo Shawa-Hidut-Tanzil, Juzuu ya kwanza ukurasa 334.
7) Tafsir At-Tustari, itwayo Ih-QaaQul-Haq, Juzuu ya tatu ukurasa 482.
8) Yanahi'ul-Mawaddah cha Al-Qanduzi Al-Hanafi ukurasa wa 51 na 140.
Na ilivyokuwa wenye kumbukumbu kwa dhahiri ya aya ni Ahlul-Kitab miongoni mwa Mayahudi na Wakristo, basi imetulazimu juu yetu kubainisha wazi kwamba wao sio waliokusudiwa katika aya hiyo Tukufu.
Kwanza; Kwa sababu Qur'an Tukufu imewataja (Mayahudi na Wakristo) mara nyingi katika aya nyingi kwamba wao waliyageuza maneno ya Mwenyezi Mungu na wakakiandika kitabu kwa mikono yao, na wakasema kuwa kimetoka kwa Mwenyezi Mungu ili wakiuze kwa thamani ndogo. na (Qur'an) imeshuhudia uongo wao na kuigeuza kwao haki, basi haiwezekani wakati huo huo iwaamrishe Waislamu warejee kwao (Mayahudi na Wakristo) katika Mas-ala wasiyoyajua.
Pili: Bukhari ameeleza katika Sahih yake ndani ya Kitabus-Shahadah mlango usemao, "Hawaulizwi washirikina". Juzuu ya tatu uk. 163.
Kutoka kwa Abuhurairah: Amesema Mtume (s.a.w.w.) "Msiwaamini Ahlil-Kitab na wala msiwapinge (kuwaambia kuwa ni waongo) semeni tumemuamini Mwenyezi Mungu na yaliyoteremshwa (toka kwake).
Hii inafundisha kutowarejea (Ahlul-kitab) katika mas-ala na (lililopo) ni kuwaacha na kuwapuuza, kwa sababu kutowaamini na kisha kutokuwapinga kunakanusha lengo la kuwauliza ambalo linasubiri jawabu sahihi.
Tatu: Bukhari ameeleza ndani ya Sahih yake katika Kitabut-Tauhidi mlango wa kauli ya Mwenyezi Mungu isemayo: "Kila siku yeye yumo katika mambo." Juzuu ya nane ukurasa 208 kama ifuatavyo:
Kutoka kwa Ibn Abbas amesema: "Enyi kongamano la Waislamu, vipi mnawauliza Ahlul-Kitab na hali kitabu chenu alichokiteremsha Mwenyezi Mungu kwa Mtume wenu (s.a.w.) ndicho chenye maelezo halisi ya Mwenyezi Mungu na hakikuharibiwa, Mwenyezi Mungu amekusimulieni kwamba Ahlul-Kitab wamekwisha badilisha na kugeuza (yaliyoteremshwa) katika vitabu vya Mwenyezi Mungu (vilivyotangulia) wakaandika kwa mikono yao kisha wakasema hayo ni kutoka kwa Mwenyezi Mungu ili wayauze kwa thamani ndogo, je hajakukatazeni yale yaliyokufikieni katika elimu kuwauliza hao? Basi fahamuni, namuapa Mwenyezi Mungu; hatujamuona mtu miongoni mwao akikuulizeni kuhusu yaliyoteremshwa kwenu."
Nne: Lau leo hii tutawauliza Ahlul-Kitab miongoni mwa Wakristo bila shaka watadai kuwa Isa ni Mungu na Mayahudi wanawapinga (Wakristo kwa madai hayo) na wala hawamkubali (Isa) japo kwa Utume, na kila mmoja wao anaupinga Uislamu na Mtume wa Uislamu, na wanasema kuwa (yeye Mtume) ni muongo na ni mzushi.
Kwa yote hayo basi haiwezekani ifahamike maana iliyomo katika aya kwamba Mwenyezi Mungu ametuamrisha tuwaulize wao, na ilipokuwa Ahlud-Dhikr katika dhahiri ya aya ni wao Ah-Lul-Kitab miongoni mwa Wayahudi na Wakristo, basi hapana shaka hali hii haikanushi kwamba aya hii imeshuka kwa watu wa Nyumba ya Mtume kama ambavyo imethibiti kwa Mashia na Masunni kwa njia sahihi. Kwa hiyo inafahamika kutoka katika aya hiyo kwamba, Mwenyezi Mungu ameirithisha elimu ya Kitabu ambacho ndani yake hakuacha kitu kwa hawa Maimamu ambao amewateua kutoka miongoni mwa waja wake ili watu wawarejee katika Tafsiri na Ta'awiili, na kwa kufanya hivyo uongofu wao utathaminiwa iwapo watamtii Mwenyezi Mungu na Mtume wake.
Kwa kuwa Mwenyezi Mungu Mtukufu na hekima yake imetukuka alitaka watu wote wawanyenyekee wateule wanaotoka miongoni mwao, ambao aliwachagua na akawafunza elimu ya Kitabu ili hali za watu ziwe katika nidhamu. Basi lau watu hawa hawangekuwepo miongoni mwa watu, nafasi ingekuwa wazi mbele ya wenye kujigamba (kuwa wanafahamu), na wajinga na hata kila mmoja angefanya kulingana na matamanio yake na mambo ya watu yangevurugika maadam kila mmoja aweza kudai kuwa ni mjuzi zaidi kuliko mwingine.

JUHUDI ZA KUPUNGUZA MIGOGORO BAINA YA MADHEHEBU YA KIISLAMU

Katika karne hii, kiasi cha miaka thelathini hivi iliyopita, baadhi ya wanazuoni wa Kishia na wasio Shia huko Mashariki ya Kati wakaona la! Hali hii ya mizozo haifai kuachwa ikaendelea. Kwa hivyo wakakutana na kujadiliana jinsi ya kuleta mkuruba na uelewano baina ya madhehebu mbali mbali ya Kiislamu - hasa baina ya Shia na Sunni. Matokeo yake yakawa ni kuundwa chama kilichoitwa Darut Taqrib Baynal Madhahibil Islainiyya na kuweka jukwaa la pamoja la kuwawezesha wanazuoni hao wa madhehebu mbali mbali kueleza imani na misimamo ya madhehebu yao juu ya mada mbali mbali za kidini.
Hatua hii ilisaidia sana kuleta uelewano kiasi cha kwamba, Sheikh Mahmud Shaltut (aliyekuwa Mufti wa AI-Azhar wakati huo) alitoa ile fatwa yake mashuhuri ya kusema kwamba madhehebu ya Ja'fari (yaani Shia Ithnaashari) ni madhehebu ya Kiislamu yanayojuzu kufuatwa katika kufanyia ibada kama madhehebu mengineo ya Sunni. Na, kwa mara ya kwanza akaruhusu madhehebu hayo yasomeshwe katika Chuo Kikuu hicho cha AI-Azhar huko Misri.
Hata hivyo, baadhi ya masheikh wa wakati huo hawakupendezwa na hatua hiyo. Miongoni mwao ni mmoja aliyekiitwa Muhibbudin al-Khatib. Huyu aliandika kitabu kwa lugha ya Kiarabu kiitwacho al-Khututul Aridhwa kuonyesha kwamba ni muhali jaribio hilo la wanazuoni wenzake kufanikiwa - hasa inapokuja kwenye uelewano baina ya Sunni na Shia - na akatoa sababu zake. Sababu hizo ndizo wanazotumia baadhi ya watu wapenda shari kuushambulia Ushia. Katika mada zifuatazo nitaonesha udhaifu na uongo wa hoja hizo za Alkhatib.

VITABU VYA HADITH VINAVYOCHAPISHWA SIKU HIZI VINACHAKACHULIWA

VITABU VYA HADITH VINAVYOCHAPISHWA SIKU HIZI VINACHAKACHULIWA KUONDOA MADAI YA MASHIA KAMA WANAVYOFANYA WAKRISTO KUONDOA ATHARI ZA UISLAMU KWENYE BIBLIA.
mengi ya matoleo mapya ya vitabu hivyo yamefanyiwa mabadiliko na baadhi ya sehemu kuondolewa, hususan zile zinazounga mkono madai ya Shia. Ufuatao hapa chini ni mfano mdogo tu wa yanayofanywa katika
vitabu hivyo:
Katika ukurasa wa 301 wa juzuu ya 3 ya Tafsir al-Kashshaaf iliyokusanywa chini ya maelekezo ya Sheikh Mustafa al-Halabi (toleo la pili, 1319 A.H. liliochapishwa na Main Government Printing House ya Amiriah Bulaq ya Misir), kuna beti zinazojitokeza ambazo kwazo Jarullah Zamakhshari, mfasiri wa al-Kashshaaf, alitangaza wazi imani yake katika
uhalali wa Ushia. Lakini katika chapisho la 1373 A.H. lililochapishwa na Printing House Istiqamah bi’l-Qahara, shairi lililotajwa halionekani tena.
Marehemu Allamah Sayyid Akhtar Rizvi katika kitabu chake Uimamu uk. 37, anaandika kushangazwa kwake kutokana na maneno yaliyoondolewa katika kitabu cha at-Tarikh cha at-Tabari, chapa ya Leiden (ya mwaka 1879 Masihia) ambayo imeyanakili maneno ya Mtukufu Mtume (s.a.w.) aliyoyatumia wakati wa karamu maarufu ya ndugu wa karibu aliyoitayarisha mwenyewe.
Maneno ya mwisho aliyoyasema Mtukufu Mtume (s.a.w.) katika karamu hiyo yalikuwa haya: “Enyi watu wangu! Huyu Ali ni ndugu yangu, wasii wangu na khalifa wangu miongoni mwenu; msikilizeni na mtiini.” Lakini katika chapa ya Misri (ya mwaka 1963 Masihia) - chapa ambayo inayodaiwa kuwa imechekiwa na ile ya Leiden - maneno haya muhimu:
“wasii wangu na khalifa wangu” yamebadilishwa na kuwa “kadha wa kadha” na kusomeka hivi: “Huyu Ali ni ndugu yangu na kadha wa kadha.” Huu ni msiba mkubwa.

UMUHIMU WA KUJIFUNZA AKIDA ZA MADHEHEBU MBALIMBALI.

Ni jambo lililo wazi na lisilopingika kuwa; dini ya Kiislamu mfano wa dini nyengine ina madhehebu tofauti, na kila dhehebu lina sifa zake katika mambo ya akida na namna ya utendaji wa amali kutokana na akida hizo wanazoziamini, lakini tofauti hizo sio kubwa kiasi ambacho pasiwe na uwezekano wa kutoshirikiana baina ya wafuasi wa dhehebu fulani na wafuasi wa dhehebu jingine, bali wafuasi hao wa madhehebu tofauti wanaweza kushirikiana na kukabiliana na fikra za watu wa kimagharibi ili kuondoa kasumba au tata zinazotolewa na watu hao kwa ajili ya kuiharifu, basi waislamu inawapasa kuihifadhi dini yao na kutowaruhusu watu hao wenye fikra hizo mbovu kufanikiwa katika malengo yao ya kuiharibu dini hiyo takatifu.
Kwa hakika kuleta mashirikiano hayo kunahitajia kutunzwa au kuadhimishwa misingi na vigezo vya kila madhehebu, na jambo la muhimu zaidi ambalo linafaa kutekelezwa ni kuwa; kila dhehebu ni lazima litambue akida ya dhehebu jingine, kwa sababu kufanya hivyo kunaweza kuzuia khitilafu zilizopo baina ya dhehebu na dhehebu, na kupatikana njia zitakazoweza kuleta mashirikiano.
Njia bora inayoweza kuyafanya madhehebu kufahamiana ni kutambuana kupitia misingi ya dini yao ya Kiislamu, na kutambuana akida zao kupitia maulamaa wao maarufu waliobobea kielimu na wanaotambulika katika jamii, kwa sababu ikiwa watafahamiana akida zao kupitia wafuasi wa madhehebu yao, wafuasi ambao hawana elimu ya kutosha inayohusiana na akida zao, na wafuasi wa madhehebu tofauti wakajenga uadui na kuwekeana chuki kutokana na ikhitilafu walizonazo, hapana shaka uadui na chuki hizoz itafunga na kuzuia njia zitakazowapeleka katika mashirikiano, na mafahamiano au mashirikiano yatabadilika na kuwafanya waislamu hao watengane kutokana na tofauti zao za kiakida na kiamali.
Hivyo ni lazima tujue akida ya Historia ya kila madhehebu kupitia kwa wenye madhehebu yao badala ya kujifunza madhehebu Fulani kupitia kwa adui yao. Tukijuana tutaheshimiana na kupendana kama waislamu.

HOTUBA ALIYOITOA MTUME (S.A.W.W) ALIPOKUWA GHARIR KHUM.

"………. Leo nimekukamilishieni dini yenu, na kuwakamilishieni neema yangu kwenu, na nimewaridhieni kwamba Uislamu ndiyo dini yenu." (Q:5:3). Baada ya Khutuba yake Mtume (s.a.w) alimtaka kila mtu kula kiapo cha utii kwa 'Ali (a.s) na kumpongeza. Miongoni mwa waliofanya hivyo ni Umar bin al-Khattab, ambaye alisema: "Hongera Ali Ibn Abi Talib! Leo umekuwa bwana wa waumini wote wanaume na wanawake."
Mwarabu mmoja aliposikia tukio la Ghadir Khum, alikuja kwa Mtume (s.a.w) na akasema: "Ulituamrisha tushuhudie kwamba hakuna mungu isipokuwa Allah na kwamba wewe ni Mjumbe wa Allah, tumekutii. Umetuamrisha kusali sala tano kwa siku, tukakutii.Umetuamrisha kufunga (saumu) mwezi wa Ramadhani, tumekutii. Kisha umetuamrisha kwenda kuhiji Makka tukakutii. Lakini hukutosheka na yote haya yote ukamnyanyua binamu yako kwa mkono wako na ukamuweka juu yetu kama mtawala kwa kusema 'Ali ni mawla wa yule ambaye mimi ni mawla kwake: je, amri hii yatoka kwa Allah au yatoka kwako wewe?"
Mtume (s.a.w) akasema: "Kwa jina la Allah ambaye ndiye Mola Pekee! Haya yanatoka kwa Allah, Mwenye nguvu na Mtukufu" Aliposikia jibu hili aligeuka na kuelekea aliko ngamia wake jike huku akisema: "Ewe Allah! Kama asemayo Muhammad ni sawa, basi vurumisha jiwe juu yetu kutoka angani na tupatie sisi adhabu kali na mateso." Kabla hajamfikia ngamia wake Allah alimvurumishia jiwe ambalo lilipiga juu ya kichwa chake na kupenyeza ndani ya mwili wake na kumuacha akiwa amekufa. Ni katika tukio hili kwamba Allah (swt) aliteremsha aya ifuatayo:
"Muulizaji aliuliza juu ya adhabu itakayo tokea. Kwa makafiri hapana awezaye kuizuia. Kutoka kwa Allah, Mola wa mbingu za daraja." (Qur'an 70:1-3) :
Wengi wa wanachuoni hawa hawakunukuu tu tangazo hili la Mtume (s.a.w) bali vile vile wanaliita sahihi: " al-Hakim al-Naysaburi, al-Mustaddrak 'ala al-Sahihyn (Beirut), juzuu 3, uk. 109-110, uk. 133, uk. 148, uk. 533. Ameelezea kwa uwazi kwamba hadithi hii ni sahihi kwa mujibu wa vigezo vya Bukhari na Muslim. al-Dhahabi alithibitisha hukumu yake.
" al-Tirmidhi, Sunan, (Cairo), juzuu 5, uk. 633.
" Ibn Majah, Sunan, (Cairo, 1952), juzuu 1, uk. 45.
" Ibn Hajar al-'Asqalani, Fath al-Bari bi Sharh Sahih al-Bukhari, (Beirut, 1988), juzuu 7, uk. 61.
" al-'Ayni, 'Umdat al-Qari Sharh Sahih al-Bukhari, juzuu 8, uk. 584.
" al-Suyuti, al-Durr al-Manthur, juzuu 2, uk. 259 na uk. 298.
" Fakhr al-Din al-Razi, Tafsir al-Kabir, (Beirut, 1981), juzuu 11, uk. 53.
" Ibn Kathir, Tafsir Qur'an al-Adhim, (Beirut) juzuu 2, uk. 14
" al-Wahidi, Asbab al-Nuzu, uk.l64.
" Ibn al-Athir, Usd al-Ghaba fi Ma'rifat al-Sahaba, (Cairo, 1932), juzuu 3, uk.92.
" Ibn Hajar al-'Asqalani, Tahhdib, (Hyderabad, 1325), juzuu7, uk. 339.
" Ibn Kathir, al-Bidayah wa al-Nihayah, (Cairo, 1932), juzuu7, uk. 340, juzuu 5, uk. 213.
" al-Tahawi, Mushkil al-Athar, (Hyderabad, 1915), juzuu 2 uk. 308-9.
" Nur al-Din al-Halabi al-Shafi'i, al-Sirah al-Halabiyya, juzuu3, uk. 337.
" al-Zrqani, Sharhe al-Mawahib al-Ladunniyya, juzuu 7, uk. 13

Swali la Kwanza kwa Mawahhabi

Kumuona Mwenyezi Mungu na Kumfanyia Mwili
Mwenyezi Mungu katika kitabu chake kitukufu anasema:"Macho hayamfikii (kumuona)". (Qur 'an, 6:103) (Hakuna chochote chenye mfano na yeye) (Qur'an 42:11).
Na anasema Mwenyezi Mungu kumwambia Musa alipotaka kumuona: "Kamwe hutaniona" (Qur'an 7:143.)
Basi ni vipi (enyi Mawahhabi) mnazikubali hadithi zilizopokewa ndani ya Sahih Bukhari na Sahih Muslim kwamba Mwenyezi Mungu Mtukufu anajidhihirisha kwa viumbe wake nao watamuona kama wauonavyo Mwezi mpevu?
Na kwamba Mwenyezi Mungu anashuka mpaka kwenye mbingu ya dunia kila usiku na ataweka unyayo wake motoni nao utajaa na kwamba ataonesha mguu wake ili waumini wamtambue na kwamba anacheka na kushangaa, na mengineyo miongoni mwa riwaya ambazo zinamfanya Mwenyezi Mungu kuwa ni mwili wenye harakati na mabadiliko, ukiwa na mikono miwili, miguu miwili na ana vidole vitano, ameziweka mbingu kwenye kidole cha kwanza, ardhi kwenye kidole cha pili, mti kwenye kidole cha tatu, cha nne maji na udongo na kwenye kidole cha tano ameweka viumbe vingine vilivyobakia na anayo nyumba anayoishi ndani yake na Muhammad ataomba ruhusa kuingia humo mara tatu.
Ametukuka Mwenyezi Mungu kwa Utukufu mkubwa kutokana na hayo (hayuko hivyo) utakasifu ni wa Mola wako Mola aliyetukuka kutokana na sifa wanazomzifu.
Jawabu la swala hili liko kwa Maimamu waongofu na Taa ziondoshazo kiza nalo ni kumtakasa kikamilifu Mwenyezi Mungu Mtukufu kutokufanana na umbile na sura na mwili na kumshabihisha na kumuwekea mpaka.
Imam Ali (a.s.) anasema:
"Sifa njema anastahiki Mwenyezi Mungu ambaye wasemaji hawafikii upeo wa sifa zake, wala wenye kuhesabu hawawezi kudhibiti neema zake, wala hawawezi kutekeleza vilivyo haki yake wenye kujitahidi, wala haziwezi kumfikia fikra zozote, na haziwezi kumtambua vilivyo akili mahiri, Mwenyezi Mungu ambaye sifa zake hazina mpaka, wala hasifiki kwa sifa za vilivyopo, na hana wakati unaohesabika wala muda wenye kikomo...
Basi mwenye kumsifu Mwenyezi Mungu Mtukufu atakuwa kamfanyia mwenzi na Mwenye kumfanyia mwenzi, kamfanyia wa pili, na Mwenye kumfanyia wa pili kamgawa mafungu, na amgawaye mafungu basi hamjui Mwenyezi Mungu. Asiyemjua hakika kamuashiria na mwenye kumuashiria kamjaalia mipaka, na mwenye kumjaalia mipaka amemuhesabu, na atakaesema yumo ndani ya kitu fulani, basi kamuambatanisha, na atakayesema yuko juu ya nini kamtoa. Yupo siyo kwa kuzuka, yupo siyo kutokana na kutokuwepo, yu pamoja na kila kitu si kwa wenza naye si kila kitu siyo kwa kumfanya si kitu, mtendaji siyo kwa harakati na vifaa, anaona wakati hakuna kinachomuona miongoni mwa viumbe wake".
Kwa hakika nimeyaelekeza macho ya wachunguzi miongoni mwa vijana wenye taaluma kwenye hazina alizoziacha Imam Ali (a.s.), zilizokusanywa ndani ya Nah-Jul-Balaghah ambacho ni kitabu madhubuti hakitanguliwi ila na Qur'an, na ni kitabu ambacho kwa bahati mbaya hakifahamiki kwa watu wengi kutokana na kampeni, vitisho na vizuizi vilivyowekwa na watawala wa Banu Umayyah na Banu Abbas dhidi ya kila kile ambacho kina uhusiano na Ali ibn Abitalib.
Sitakuwa nimezidisha nitakaposema kwamba ndani ya Nahjul-Balaghah kuna elimu nyingi na mafunzo mengi ambayo watu (wataendelea) kuyahitaji siku zote, na ndani ya Nahjul-Balaghah kuna elimu ya akhlaq, elimu ya jamii, uchumi na miongozo madhubuti katika elimu za dunia na teknolojia na zaidi ya hapo kuna falsafa, tabia, siasa na hekima.
Kwa hakika nimeyathibitisha hayo mimi mwenye we ndani ya Insha niliyotoa kwenye Chuo Kikuu cha Sirbun, Insha ambayo ilijadiliwa juu ya maudhui nne nilizozichagua kutoka ndani ya Nahjul-Balaghah na kutokana na maudhui hizo nilipata shahada ya "Udaktari".
Basi lau Waislamu wangeifuata Nahjul-Balaghah kikamilifu wakayachambua mas-ala yote yaliyomo na kila nadharia, bila shaka (Nahjul-Balaghah) ni bahari yenye kina kirefu, kwani kila aizamiapo mtafiti hutoa ndani yake Lulu na Marjan.
TA'ALIQ (Ufafanuzi): 
Iko tofauti iliyo wazi kati ya Aqida mbili:
Aqida ya Ahlus-Sunnah Wal-Jamaa ambayo inamfanya Mwenyezi Mungu Mtukufu kuwa na mwili, umbo na sura kama kwamba yeye ni mtu anayetembea na anashuka (kutoka juu) na mwili wake unahifadhiwa na anayo nyumba (anamoishi) na mengineyo miongoni mwa mambo yanayochukiza.
Mwenyezi Mungu ametakasika mno, yu mbali na mambo hayo.
Aqida ya Mashia ambao wanamtakasa Mwenyezi Mungu na kutomfananisha na kumfanyia mwili, na wanasema kuwa haiwezekani kabisa kumuona (Mwenyezi Mungu) hapa duniani wala akhera. Nami binafsi naamini kwamba riwaya wanazotolea hoja Ahlus-Sunnah Wal-Jamaa zote ni uchafuzi wa Myahudi katika zama za Masahaba, kwani Kaabul-Ahbar Myahudi ambaye alisilimu katika zama za Omar bin Al-Khatab ndiye aliyeingiza itikadi hizi ambazo Wayahudi wanaziamini (na alifanikiwa kwa) kupitia njia za baadhi ya Masahaba wepesi (wa kuhadaika) kama vile Abu-Hurairah na Wahab ibn Munabbah.
Basi ziko riwaya nyingi za aina hiyo zilizopokelewa ndani ya Bukhari na Muslim kutoka kwa Abu-Hurairah, na imekwishatangulia katika uchunguzi uliopita namna gani Abu-Hurairah asivyotenganisha hadithi za Mtume na hadithi za Myahudi Kaabul-Ahbar kiasi kwamba Umar bin Khatab alimpiga na kumzuwia asisiimulie riwaya kuhusu suala la Mwenyezi Mungu kuumba mbingu na ardhi katika siku saba.
Na madam Ahlis-Sunnah Wal-Jamaa wanaziamini Sahih Bukhari na Muslim na kuvifanya kuwa ni vitabu sahihi mno, na maadam hawa wanamtegemea Abu-Hurairah kiasi kwamba amekuwa ndiyo tegemeo la wanachuoni wa hadithi (wa Kisunni) na yeye (Abu-Hurairah) kwa Masunni ndiyo mpokezi wa Uislamu (katika hadithi). Basi kwa hali kama hii haiwezekani kwa Masunni kubadili itikadi yao isipokuwa kama watajikomboa kutokana na kufuata kiupofu, na wakarejea kwa Maimamu waongofu (ambao) ni kizazi cha Mtume nao ndio mlango wa mji wa Elimu ambao huendewa.
Wito huu hauwahusu Wazee na Masheikh, bali kijana mwenye taaluma miongoni mwa Masunni, pia ni miongoni mwa wajibu alionao (kijana) ni kujinasua kutokana na kufuata kiupofu na afuate hoja na dalili.